powered by
send-it.me

Adventist World-Kiswahili inamshukuru kila aliyejiandikisha kwa ajili ya jarida hilo, kupitia kwa jukwaa letu la awali, yaani chaneli ya WhatsApp. Tumefurahia kupokea jumbe kutoka kwako, na vilevile shuhuda za jinsi umetumia jarida hili linalotia moyo kuwafikia wengine kwa ajili ya Kristo!

Tungependa ujue kuwa tulihamia jukwaa jipya tangu Februari 2024. Zaidi ya yote, tungependa uhame pamoja nasi. Adventist World-Kiswahili haitaki kumwacha nyuma yeyote aliyejiandikisha.

 

Badala ya kupokea ujumbe wa WhatsApp pamoja na toleo jipya kila mwezi, sasa tunakupa kiungo kwa tovuti ya bure ambayo ni nzuri kwa simu, ambapo unaweza kuyasoma makala yote, kama kawaida. 

Pia tutakiweka kiungo hicho kwenye ukurasa wa Facebook wa Adventist World-Kiswahili kila mwezi, ambapo unaweza kututumia jumbe na taarifa kuhusu jinsi makala hii inakufaidi wewe na jamii yako. Pia unaweza kututumia maoni na mapendekezo jinsi ya kuifanya makala hii iwafae zaidi wasomaji!

Ukipenda, unaweza kutuma baruapepe: 
kwambokaj@ecd.adventist.org ukiwa na maswali yoyote.

 

Moja ya manufaa ya tovuti mpya ya Adventist World-Kiswahili ambayo ni nzuri kwa simu, ni kwamba kutakuwa na lugha zingine nyingi za kuchagua, ikiwa ungependelea Kiingereza au lugha nyingine yoyote, unaweza kuangalia kama ipo, kando na ile ya kawaida ya Kiswahili.

 

Manufaa mengine ni kwamba ni rahisi kushiriki kiungo hicho kipya cha Adventist World-Kiswahili, kwa marafiki na familia. Tunakuhimiza ufanye hivyo. Hebu iangalie sasa hivi.

 

Tunatumai kuwa na uhusiano mrefu na wa furaha na wasomaji wetu wa Adventist World-Kiswahili.

 

Mungu akubariki,

 

Timu ya Adventist World-Kiswahili

Tunaamini katika nguvu ya maombi, na tunakaribisha hitaji la maombi ambayo tutashiriki katika ibada ya watendakazi kila Jumatano asubuhi. Tuma maombi yako kwa kwambokaj@ecd.adventist.org, na utuombee tunapofanya kazi pamoja kuendeleza ufalme wa Mungu.

 

Picha ya jalada: sezer66 / iStock / Getty Images Plus  / Getty Images 

Iwe ni katika utawala, uongozi, jamii ya kiraia, au hata malezi, matokeo mazuri hutokea ikiwa upo uwiano wa ukali na upole. Ukali hujumuisha kanuni, sheria, haki, utaratibu, uaminifu, utulivu, umuhimu, na nidhamu; upole ni, msamaha, uelewa, huruma, werevu, mapatano, na wema. Uwiano sahihi unaweza kuzuia kuvuka mipaka: ukali sana husababisha vitu kuvunjika, wakati upole kupita kiasi hauleti mafunzo, mabadiliko, au maendeleo. Ni kwa jinsi gani, basi, uwiano huu unaweza kupatikana?

 

Kwa mfano, labda umekamatwa na polisi kwa kosa dogo la barabarani. Ukali huwasilishwa mbele yako: sheria. Uwiano hapa ungekuwa kulipa adhabu inayolingana na kosa dogo. Lakini ikiwa ulikuwa unapita kwa kasi kwa sababu ulikuwa unamharakisha mwanamke mjamzito hospitalini, upole ungewasilishwa kusawazisha ugumu, ili kuleta uwiano. Ikiwa sheria ingekuhitaji kupoteza vidole vyako kutokana na taa ya nyuma ya gari iliyovunjika, hii isingekuwa na uwiano. Ikiwa sheria ingehitaji kuomba msamaha tu baada ya kusababisha ajali ya magari 14 barabarani, hii pia isingekuwa na uwiano.

 

Kupata huu uwiano sahihi kumekuwa lengo kuu la historia ya kisheria. Uwiano umetafutwa na dini za kipagani, sayansi za kijamii za kisasa, na wanafalsafa wa kila enzi. Wanaoamini sayansi na maendeleo wamepinga swali hilo linalochukiza. Utamaduni maarufu unatufurahisha kwa kuwasilisha yaliyovuka mipaka. Lakini Ukristo una kielelezo cha wazi kabisa cha uwiano wa ukali na upole. Katika uelewa wake wa simulizi ya pambano kuu, Uadventista (huenda) unawasilisha uwiano huu mkubwa katika mwanga wake mpana, kutoka katika mtazamo wa kiulimwengu.

 

Msalaba wa Kristo ndipo mahali ambapo mivutano inafikia kilele chake. Ni ufunuo kamili wa mema na mabaya. Ndipo mahali ambapo amani na maumivu hukaa pamoja. Ni wokovu na hukumu. Ni uzuri na utisho; fahari na kashfa; utukufu na mateso. Kifo cha Yesu kinaonyesha ugumu katika kudumisha haki ya Mungu, lakini pia urahisi unaonyesha upendo wa Mungu kwa binadamu. “Fadhili na kweli zimekutana, haki na amani wamehusiana” (Zab. 85:10).

 

Kwa kutafakari juu ya msalaba, wazazi wanaweza kupokea ufahamu na subira ya kukaripia kwa upendo, kwa uwiano. Makanisa yanaweza kupokea ustahimilivu na moyo wa Kristo wa kuadhibu washiriki wake kwa nia ya ukombozi. Konferensi inaweza kuonyesha usawa, lakini pia huruma, katika kushughulika na wachungaji na makanisa. Union zinaweza kuiishi amri na tabia ya Kristo katika kusimamia taasisi. Konferensi Kuu na divisheni zake zinaweza kuwa na uadilifu mkubwa na wenye huruma zaidi katika kuongoza utume wa Kristo hadi mwisho wa dunia.

 

Uwiano huu haupatikani ndani. Haupatikani katika maarifa, tamaduni, au uzoefu. Chanzo chake kinapatikana katika msingi mkuu nje: msalaba wa Kristo, wenye ukali na upole.

Huko Zambia, makundi ya Maranatha Volunteer International watembelea maeneo kadhaa ya visima, wakitathmini kwanza visima vilivyoko ambavyo huduma hiyo ilisaidia kuvichimba na kurudisha sehemu zinazohitajika. Kupata maji bure kunaongeza fursa kwa ajili ya maendeleo ya jamii na utume nchini kote.

Zaidi ya 1,600

Idadi ya watu waliokusanyika kwenye tamasha la muziki lenye mada ya Krismasi lililoandaliwa na Kanisa la Waadventista wa Sabato Quisqueya-Kati huko Santo Domingo, Jamhuri ya Dominika, katika Ukumbi wa Sambil Event mnamo Desemba 21. Tukio hilo la bure lililotumia saa mbili na nusu, lenye kaulimbiu ya “Nyota ya Matumaini,” lilikuwa tukio lenye matokeo makubwa kwenye jamii lililoandaliwa na kanisa hilo mwaka wa 2023 na ni mara ya kwanza katika miaka 15 ambapo kanisa limefanya tukio la uinjilisti nje ya hekalu lake ili kuwafadhili watu zaidi katika jamii.

Miaka 120

Muda wa utume wa Waadventista ambao umekuwa ukilenga Korea Kusini. Union Konferensi ya Kikorea inalenga kutumia kumbukumbu hiyo kama kichocheo cha kurejesha nguvu za umishonari. Mfululizo wa shughuli mbalimbali za kumbukumbu za miaka 120 ya utume nchini humo imepangwa kwa mwaka 2024. Ndani ya tukio la kumbukumbu na juhudi zake, lengo kuu linazingatia shukrani, heshima, kufufua misheni, na kujiandaa kwa ajili ya siku za usoni.

Mitandao ya Kijamii

Hivi karibuni washiriki wa Kanisa la Waadventista wa Sabato waliulizwa ikiwa ilikuwa vigumu kuacha kutumia mitandao ya kijamii walipotaka kufanya hivyo.

Zaidi ya 250

Umbali kwa kilomita ambazo Henry Smith, mwanachama wa Huduma za Vijana Waadventista, pamoja na Watafuta Njia Millicent Anna Stella Asane na Lawrence Manful walitembea ili kuhudhuria Mkutano wa Nne wa Watafuta Njia wa Union ya Afrika Magharibi-Kati, uliofanyika Desemba 24-30. Wakianza safari Desemba 21, watu hao watatu walitembea zaidi ya kilomita 250 (takribani maili 155), na kufika kwenye sherehe ya ufunguzi ya mkutano huo Desemba 25. Safari hii, iliyoongozwa na Smith, imekuwa ni desturi tangu mwaka 1996, na lengo lake ni kutafuta fedha kwa ajili ya mayatima.

“Tulitiwa moyo, tulineemeshwa na kutiwa nguvu. Kituo hicho kilikuwa ni kichocheo cha kuendeleza mazungumzo kuhusu huduma ya vijana wakubwa katika Union yetu . . . ili kuwajulisha kuhusu vijana hawa wa ajabu wanaojitokeza wenye shauku na mwamko kuhusu imani yao.”

—Gregory Taylor, mkurugenzi wa huduma za vijana na vijana wakubwa wa Union Konferensi ya Kusini, kuhusu kituo cha tatu cha Ziara ya MAISHA ya Vijana Wakubwa katika Divisheni ya Kaskazini mwa Marekani (NAD). Tukio hilo lilifanyika katika kanisa la Spring Meadows huko Florida kati, Marekani, na ni mfumo wa uanafunzi wa vijana wakubwa wa NAD, ukiwa na lengo la: Matokeo ya Uongozi, Uhusiano wa baina ya Vizazi, Maendeleo ya Imani, na Huruma ya Kila Siku.

“Nimepata heshima kushiriki katika tukio la kumbukumbu ya miaka 100 ya Seminari na Chuo cha Kiadventista cha Pakistan. Kupitia mashindano ya Kengele ya Dhahabu kuhusu kitabu cha Pambano Kuu, nilihisi shauku ya vijana wa Pakistani ambao wanapenda Neno la Mungu. Na sherehe ya ubatizo wa pamoja siku ya Sabato mchana ilikuwa ni uzoefu usiosahaulika.”

—Ho Young Choi, mkurugenzi wa vijana wa Divisheni ya Kaskazini mwa Asia-Pasifiki, kuhusu tukio la uamsho lililofanyika mwishoni mwa Novemba katika Seminari na Chuo cha Kiadventista cha Pakistan katika wilaya ya Sheikhupura, Punjab. Zaidi ya watu 700 walikusanyika kila jioni katika kanisa la chuo kikuu. Mwishoni mwa tukio hilo, watu 148 walibatizwa. Mafanikio haya yanatarajiwa kuchangia zaidi ya ubatizo wa watu 2,000 nchini Pakistani ndani ya mwaka mmoja, ambao ungekuwa wa kwanza katika historia ya nchi hiyo.

120

Idadi ya miaka tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Kiadventista cha Washington (WAU). Shule hiyo ilianzishwa mwaka 1904 huko Takoma Park, Maryland, Marekani. Katika miaka yote, shule imejitoa kabisa kwa ajili ya elimu, imani na jamii. Ili kuadhimisha tukio hili kuu, shule imepanga matukio na shughuli mbalimbali mwaka mzima, ambayo yataiwezesha jamii ya WAU kukusanyika pamoja na kusherehekea urithi wa huduma, uongozi, na imani wa chuo kikuu.

“Shauku yake na kujitoa kwake vilidhihirika na upendo wake na bidii vilimfanya apambane kwa ajili ya ustawi wa (wanawake). Alipambana kuwawezesha wanawake ulimwenguni kote kuwa na nguvu kiroho, kihisia, na kimwili ili kuleta kizazi bora cha wanawake kwa utukufu wa Mungu.”

—Dinorah Rivera, mkurugenzi wa zamani wa huduma za wanawake katika Divisheni ya Marekani-Kati, kuhusu kazi ya Heather-Dawn Small. Small, kiongozi wa wanawake Waadventista wa muda mrefu na mtetezi, alifariki Januari 2 kutokana na kansa. Kwa miongo kadhaa, Small alihudumu katika Kanisa la Waadventista kwa nyadhifa mbalimbali. Alihudumu Trinidad na Tobago kama msaidizi wa rais wa Chuo Kikuu cha Kusini mwa Caribbean na huduma za watoto na baadaye kuwa mkurugenzi wa huduma za wanawake katika Union Konferensi ya Caribbean. Small alikuwa mkurugenzi mwenza wa huduma za wanawake katika Konferensi Kuu mnamo mwaka 2001 na alichaguliwa kuwa mkurugenzi mnamo mwaka 2005, nafasi ambayo aliishikilia hadi wakati wa kifo chake.

Miradi kadhaa ya siku za hivi karibuni ya Nyumba ya Uchapishaji ya Korea (KPH), iliyopo Korea Kusini, inaonyesha msaada wake kwa juhudi za utume wa Kiadventista, viongozi kutoka Divisheni ya Kasikazini mwa Asia-Pasifiki (NSD) ya Kanisa la Waadventista wa Sabato hivi karibuni walisema.

 

Tarehe 2 Desemba 2023, wakati wa ibada ya Sabato ya maadhimisho ya miaka 100 ya Seminari na Chuo cha Kiadventista cha Pakistan, viongozi waliweka wakfu mfululizo wa masomo ya unabii na yale ya kujifunza Biblia ya Kiurdu. Kwa msaada wa KPH, juhudi hizi na nyinginezo zinasaidia kuleta injili kwa watu wanaozungumza Kiurdu katika Asia Kusini na hasa Pakistan, ambako Kiurdu ni lugha ya kitaifa, inayozungumzwa na zaidi ya watu milioni 200.

 

KPH pia ilisaidia usambazaji wa nakala 10,000 za Njia Salama na nakala 3,000 za Tumaini la Vizazi Vyote, zote zilizoandikwa na mwanzilishi mwenza wa Kanisa la Waadventista Ellen G. White. Mradi wa awali ulifadhiliwa kama sehemu inayojitegemea ya nyumba ya uchapishaji, huku mradi wa pili ukiwa juhudi shirikishi pamoja na washirika wa huduma za utume zikiwemo gharama za utafsiri na uzalishaji, pamoja na uchapishaji na usafirishaji, viongozi waliripoti. Kujihusisha kwa KPH nchini Pakistan siyo jambo geni, kwa vile nyumba ya uchapishaji katika matukio ya nyuma ilituma machapisho ya Kiadventista nchini Pakistan, nchi ambayo watu wengi ni wa imani ya Kiislamu.

 

Mkuu wa Seminari na Chuo cha Kiadventista cha Pakistan Gee Sungbae alisema mwitikio umekuwa mzuri mno. Alikazia umuhimu wa Njia Salama, akieleza kwamba ni “ujumbe muhimu unaotambulisha kiini cha Ukristo kwa Waislamu wanaoonyesha shauku ya kujua.” Lengo la kitabu hiki ni kuwaongoza Wakristo, Waadventista walioimarika na waongofu wapya, mbali na imani zilizochanganywa na utamaduni na kuelekea kwa ufahamu wa kweli wa asili ya Ukristo, Sungbae alisema.

 

“Tumaini la Vizazi Vyote kitasambazwa miongoni mwa viongozi mahalia wa Waadventista na Waprotestanti na kutumika kama mwongozo wa kujifunza Biblia chuoni,” aliongeza.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa KPH Nam Soo-myung pia alisisitiza uwezo wa kimishonari wa rasilimali zilizotolewa. “Nina imani vitabu hivi vitatumika kama chombo chenye nguvu cha kueneza injili katika nchi kama Pakistan,” Nam alisema. “Kwa kuendelea, KPH inapanga kuunga mkono uinjilisti kikamilifu. Ninaomba makanisa yote na waumini waweze kuvutiwa na kujitoa katika mpango huu.”

 

Sambamba na KPH, wafadhili binafsi walitoa kwa ukarimu nakala 1,000 za mfululizo wa masomo ya Biblia ya Imeandikwa. “Nyenzo hizi zimetengenezwa kama miongozo ya masomo kwa wamishonari, wachungaji, na washiriki wa kanisa wenye mafunzo,” Sungbae alisema. “Ninatumai nyenzo hizi zitathibitisha kuwa tunu kwa mipango ya uinjilisti, kwani watu wa Pakistan wengi wana hamu ya kuchunguza Biblia.”

 

NSD iliijumuisha Pakistan hivi karibuni kama sehemu ya eneo lake, baada ya ombi lililopitishwa kutoka kanda hiyo kwenda Konferensi Kuu (GC) mwaka wa 2022. Mnamo Oktoba 8, 2023, katika Kikao cha Mwaka cha Kanisa la Waadventista huko Silver Spring, Maryland, wajumbe wa Kamati Tendaji ya GC (EXCOM) walipitisha kuunga mkono mabadiliko hayo.

 

Pakistan, taifa lenye Waislamu wengi Kaskazini-Magharibi mwa bara la Hindi, lilipata uhuru kutoka katika utawala wa Waingereza mwaka 1947. Eneo hilo awali liligawanywa katika Pakistan ya Mashariki na Pakistan ya Magharibi. Mnamo 1971, Pakistan ya Mashariki ilipata uhuru kama Bangladesh, huku Pakistan ya Magharibi ikiwa ile inayojulikana sasa kama Pakistan. Ikiwa na idadi ya watu milioni 240, inasimama kama nchi ya tano yenye watu wengi zaidi duniani. Kwa mujibu wa takwimu, karibu asilimia 97 ya wakazi wake ni Waislamu, ikiwaacha Wakristo kama kikundi cha watu wachache, ikiwa ni pamoja na chini ya Waadventista 20,000 waliobatizwa.

Juma la kwanza la mwezi Septemba 2023 halikuwa tu juma la kawaida kwa wanawake wengi Waadventista katika Divisheni ya Bahari ya Hindi-Kusini mwa Afrika (SID). Zaidi ya wanawake elfu mbili kutoka Union sita za Kanisa la Waadventista wa Sabato nchini Malawi, Zambia, na Zimbabwe walihudhuria mkutano wa kanda katika Chuo Kikuu cha Rusangu karibu na Monze, nchini Zambia. Mia mbili na tisini walitoka katika Union Konferensi ya Malawi. Mada ya mkutano huo wa kanda ilikuwa “Bora, Sio Chungu.”

 

Margery Herinirina, mkurugenzi wa huduma za wanawake wa SID, alikuwa mzungumzaji mkuu nyakati za ibada. Alishiriki pamoja na wajumbe neno la Mungu kutoka kitabu cha Ruthu 1:20 na 2:11. “Ni vizuri kwa wanawake kuwa wema, sio wachungu, kwani uchungu ni kama sumu katika moyo wa mtu inayoondoa mawazo mazuri,” alisema. Zaidi aliwahimiza wanawake kuwa na tumaini kila wanapokabiliana na changamoto.

 

“Unapaswa kujenga imani kwa Mungu na utabadilishwa,” Herinirina alisema. Aliendelea kwa kuwahimiza wanawake kutendeana wema ili baadhi ya watu wabadilike na kuanza kumtegemea Mungu kupitia wema wao.

 

Mwenyekiti wa SID Harrington Simui Akombwa alihudhuria. Akombwa alisema ni wakati mwafaka kwa wanawake kuinuka na kuangaza kwa jina la Bwana. “Tuko katika ulimwengu uliojaa changamoto, lakini tuinuke, tuangaze, na kuomba,” alisema. “Na changamoto zitatoweka.”

 

Viongozi wengine waliwasilisha mada mbalimbali. Mkurugenzi wa uwakili wa Union Konferensi ya Zimbabwe-Mashariki Trymore Mutimwii alizungumza kuhusu wanawake na uinjilisti. Gift Mweemba, Mchungaji mstaafu na kiongozi wa Unioni Konferensi ya Kusini mwa Afrika, pia aliwatia moyo washiriki kuwa bora na sio wenye uchungu. “Wanawake wanapaswa kujithamini kwa sababu wao ni nafsi inayojitegemea,” Mweemba aliwaambia waliohudhuria. “Unapaswa kujiamini kwamba unaweza kufanya vizuri zaidi. . . . Jionee fahari, kama Yesu Mwenyewe alivyomwamini mama yake alipokuwa duniani.”

 

Precious Milingo, mshiriki wa kanisa la Waadventista wa Sabato Olive huko Kampala, Uganda, na mwanzilishi wa Utano Health Solutions, aliwaongoza wageni katika masuala yanayohusiana na afya ya wanawake. Mkurugenzi mtendaji katika Benki ya Akiba ya Malawi, Mercy Kumbatira, aliwasilisha mada ya wanawake na fedha. Kuhusu wanawake na unyanyasaji, Maimba Ziela, meneja mwenza katika chama cha Lusitu na mkurugenzi wa huduma binafsi katika Unioni Konferensi ya Kaskazini mwa Zambia, alishauri, “Usijifiche au kunyamaza unaponyanyaswa. Tafadhali tafuta msaada.” Na kuhusu wanawake wenye shughuli nyingi na usawa wa kazi, Linda Sibanda, mkurugenzi wa huduma za wanawake wa Union Konferensi ya Kaskazini mwa Zambia, alishauri wanawake kukuza ujuzi wa kusimamia muda. “Jifunze kuthamini wanaokuzunguka na ushirikiane nao kama timu ili kuepuka mavune,” alishauri. “Na jifunze kusema hapana.”

 

Nokanyo Lulu Ndlovu, kutoka Afrika Kusini, alikuwa mzungumzaji mkuu wakati wa saa ya ibada kila siku na ibada ya jioni. “Hebu tuchague tumaini na shukrani badala ya uchungu wakati wowote tunapokuwa na changamoto,” Ndlovu alisema. “Tumshukuru Mungu kwa kila jambo na tuandike mambo mema ambayo Bwana ametutendea. Tunapoishi katika maombi, tutakuwa na shukrani na watoto wetu wataiga.” Wakati wa tukio hilo, wanawake walitoka kwenda kutembelea. Walitembelea Hospitali ya Misheni ya Monze, Gereza la Monze, na shule ya watoto wenye ulemavu ya Choongo. Wanawake waligawa vitu mbalimbali kama vile sapatu, sabuni, vitabu, na pesa taslimu.

 

Mkutano huo ulidumu kwa siku nne na ulifungwa na magwaride ya union pamoja na maonyesho ya utamaduni.

Shirika la Kiadventista la Maendeleo na Misaada (ADRA) nchini Canada hutoa misaada ya dharura na maendeleo kote ulimwenguni. Kwa sehemu kubwa, shirika hilo ni kioo na uenezi wa Kanisa la Waadventista wa Sabato duniani kote. Sio tu ofisi za ADRA katika zaidi ya nchi 100 zinazofanikisha kazi ya ADRA; pia jumuiya pana ya kanisa ambayo inaunda na kutoa maono ya jinsi kuzihudumia jamii zetu kunavyoweza kuonekana.

 

Vijana wakubwa na vijana wadogo wa Kanisa la Waadventista wa Sabato nchini Canada walitoa maono ya jinsi ambavyo ingekuwa tunu kuleta mabadiliko nyumbani. Maono yao: kufanya kazi kwa ajili ya kuboresha maisha ya watu kwa njia ambazo ziligusa mahitaji yao halisi. Kutokana na maono haya lengo liliibuka: kufanya kitu ili kuwasaidia wenyeji kwa njia dhahiri, ya vitendo, na isiyo ya hila ambayo inakuza uhusiano wa kweli na urafiki.

 

Kipindi cha mwaka 2023, makundi manne ya vijana Waadventista waliojitoa kwa hiari walisafiri kwenda katika jamii anuai za wenyeji kaskazini mwa Ontario. Uhusiano wa muda mrefu wa ADRA na shirika mwenza katika eneo hilo, ambalo ni Independent First Nations Alliance (IFNA), ulitoa fursa kwa makundi haya ya Waadventista kushirikiana na wenyeji kufanya kazi ya maana na ya kivitendo juu ya kuzuia moto na usalama wa moto. Hii ni mada ya muhimu sana kwa watu wengi wa Canada, hasa baada ya mwaka wa moto mkubwa wa ghafla.

 

Pamoja na meneja wa zamani wa Canada wa programu za kitaifa za ADRA, Daniel Saugh, na wakala wa kidijitali wa harambee na mwana mikakati wa mitandao ya kijamii, Randy Sidaoui–ambao wote waliongozana na kundi huko Whitesand–timu za vijana wakubwa wa Kiadventista zilihudumia mahitaji na mipango iliyokuwa ya muhimu kwenye hifadhi hizi. “Lengo letu la msingi lilikuwa kusimama kwa umoja pamoja na jumuiya ya wenyeji, kufanya kazi katika uzuiaji, kinga, na msaada wa uokoaji dhidi ya moto,” Sidaoui alisema. “Pia ilikuwa fursa ya kujifunza kutoka kwa wenyeji kuhusu mbinu zao za thamani na mbinu za utunzaji wa ardhi zinazofahamika. Timu yetu yenye shauku ilisaidia kuweka ving’ora vya moto katika nyumba ambazo hazikuwa navyo na kusafisha pamoja na kuondoa mabaki mengine kutoka kwenye vizuia moto.

 

Timu hiyo pia ilikagua ving’ora vya moto vilivyowekwa hapo awali ili kuhakikisha kuwa vyote bado vinafanya kazi, na timu ilifanya kazi mbalimbali kama ilivyohitajika ili kusaidia wafanyakazi wenyeji: kusafisha malori na kituo cha zimamoto; wakihesabu na kusasisha taarifa za nyumba katika eneo hilo ili kuongeza ufanisi wa kukabiliana na maafa; na kuwapa wafanyakazi chakula kama kitendo cha kuonyesha urafiki.

 

Kabla ya kufanya kazi pamoja na watu kutoka katika mataifa haya, washiriki wa timu walipata mafunzo ya uhamasishaji. Waandaaji waliwahimiza kuchukua programu ya mafunzo ya Misimu minne ya Upatanisho ambayo iliundwa na Chuo Kikuu cha First Nations na kupatikana kupitia ofisi ya huduma kwa wenyeji ya Kanisa la Waadventista wa Canada. Nyenzo hizi za mafunzo zilisaidia kuhakikisha kwamba utendaji kazi kati ya wafanyakazi wa kujitolea wa Canada na wenyeji ulikuwa wa heshima na amani kwa namna yoyote ile.

 

“Ilikuwa safari ya ajabu ambapo tulikutana na watu wa ajabu na wakarimu,” Sidaoui aliongeza. “Vijana wengi tuliokutana nao wanajali sana jamii yao na wanafanya kazi kwa bidii ili kulinda watu wanaowazunguka.” Kwa Sidaoui, “ilikuwa baraka halisi na uzoefu wa kujifunza kuwa miongoni mwa wenyeji kwa muda wa juma moja, kushiriki chakula pamoja nao na kushiriki katika moja ya sherehe zao za utamaduni. Sehemu bora zaidi ya uzoefu huu ilikuwa mapokezi ya furaha tuliyopokea katika jamii na nafasi ya kutengeneza kile ambacho tulitarajia kingeweza kuwa urafiki mpya wa kudumu,” alisema.

Wanandoa wachanga Waadventista wa Sabato kutoka Meksiko walianzisha njia ya kuvutia ya kufuata nyayo za Yesu: kwa kushiriki safari yao waliyoitamani sana kwenda Nchi Takatifu kupitia kile ambacho kimekuwa kipindi cha televisheni kwenye Hope Channel ya Marekani-Kati.

 

Wakati César Martínez mwenye umri wa miaka 30, na Gaby Chagolla, 26, walipofunga ndoa mwaka 2019, walikuwa na ndoto moja: kufurahia fungate kwa kusafiri kwenda Nchi Takatifu huko Israeli. Walipogundua kwamba hawakuwa na fedha za kutosha wakati huo, walitulia katika kazi zao na kuweka akiba yao. Wenzi hao walihama kutoka Tuxtla Gutiérrez, Chiapas, na kuanza kazi mpya. Usiku mmoja mwaka 2021, walipokuwa wakisoma kitabu cha Yohana pamoja na marafiki, César na Gaby walihisi kutiwa moyo kwa mara nyingine tena juu ya kutembelea Yerusalemu na maeneo yanayoizunguka. Walihisi kwamba ilikuwa ndoto ambayo inaweza kufikiwa, na wakaamua kuiweka mikononi mwa Mungu.

 

“Tulijua kwamba hatukutaka tu kuwa na uzoefu wa kiroho kwa ajili yetu wenyewe bali kushiriki na wengine,” César alisema. Wakapanga mpango. Wangefanya safari na kuionyesha kwenye chaneli ya YouTube ya Gaby Séptima Estación kwa jina Septima Estación (Kituo nambari 7). Katika kituo hicho, kwa kawaida hushiriki mafungu ya Biblia, masomo ya kiroho, na jumbe chanya kwa wafuatiliaji wake zaidi ya 30,000. “Tulitaka kuhakikisha kwamba maudhui yanawafikia watu wengi,” Gaby alisema.

 

César alikubali. “Tulipoendelea kuombea ndoto yetu, mtindo wetu wa maisha ulibadilika,” alisema. “Tulianza kuweka akiba ya fedha, tukafikiri tofauti kuhusu matumizi yetu, tukimtumaini Mungu.”

 

Baada ya mwaka wa kuweka akiba kwa kadiri walivyoweza, walinunua tiketi zao. Tiketi zilipopatikana, walianza kufanya utafiti zaidi wa safari yao na kuja na maudhui ya kushiriki. Pase de Abordar (Hati ya Ruhusa) ndilo jina walilokuja nalo kwa ajili ya safari yao huko Yerusalemu.

 

Walipoanza kufikiria juu ya kuwafikia watu mtandaoni, waliwaza, “Kwa nini tusiwafikie watu wengi zaidi?” “Tuliielezea kwa viongozi wa Hope Channel Marekani-Kati, na walilipenda wazo hilo, na njozi nyingine ikaundwa–kutengeneza kipindi cha televisheni,” Gaby alisema.

 

Novemba 2022, walisafiri hadi Yerusalemu na kurekodi matukio sita walipotembelea Galilaya, Bethlehemu, Bustani ya Gethsemane, na maeneo mengine maarufu katika Biblia.

 

“Tuliposafiri, tulishiriki na watazamaji wetu wa mitandao ya kijamii kila hatua ya safari yetu, na mwitikio kutoka kwa watu wengi ulitugusa sana,” Gaby alisema.

 

Uzoefu wao wa kusafiri ulijumuisha nyakati nyingi bora. “Hakuna kitu kizuri zaidi kuliko kuona mahali ambapo Yesu alienda na kuona ushahidi huo wa uthibitisho wa kihistoria unaotajwa katika Biblia,” César akasema. Kwa Gaby, kuikaribisha Sabato ya siku ya saba mbele ya Ukuta wa Sulemani katika Jiji la Kale la Yerusalemu na kutembelea kanisa la karibu zaidi la Waadventista wa Sabato ni jambo lisilosahaulika. “Tulishiriki katika karamu nzuri ya kiroho na kusifu siku ya Sabato,” Gaby alisema.

 

Mwitikio wa Pase de Abordar umekuwa baraka kweli, Gaby alisema. “Watu wametushukuru, wameshiriki kwamba wametazama kila kipindi pamoja na wafanyikazi wenzao, marafiki na familia.”

 

Pase de Abordar ni kipindi cha kwanza ambacho ni kipindi cha vitendo zaidi, kijamii, kipindi kinacholenga vijana kwenye Hope Channel Marekani-Kati, Abel Márquez, mkurugenzi mtendaji wa Hope Channel Marekani-Kati, alisema. “Tunajifunza kutokana na uzoefu wao, kwa sababu ni wenzi wa ndoa wanaotaka kushiriki ujumbe wa upendo na tumaini unaopatikana kwa Yesu.”

Biblia inatoa miongozo ya jinsi tunavyopaswa kuhusiana sisi kwa sisi katika ngazi yoyote ile. Kurejesha wenye dhambi, bila kujali ukubwa wa kosa, kwa uhusiano unaookoa na Kristo ni jambo ambalo kanisa lazima lifanye1. Ukweli huu unaonyeshwa katika nyanja mbalimbali za mafundisho ya Kristo, kwani maisha na mafundisho yake yalilenga wokovu. Kwa mfano, alipoulizwa kwa nini alikuwa akishirikiana na wale ambao walitazamwa kuwa si waaminifu katika biashara (watoza ushuru) na waliotengwa (wenye dhambi) katika jamii, alijibu bila shaka kwa kuangazia madhumuni ya utume Wake–yaani, kuwaokoa wenye dhambi (Luka 5:31, 32). Kwa hiyo, hii inafafanua kusudi la kuwepo kwa kanisa: kutoa mazingira wezeshi kwa ajili ya kufanywa upya au kuimarisha uhusiano na Kristo kupitia jumuiya.

 

Mathayo 18 inatupatia baadhi ya hatua kielelezo ili kuongoza juhudi zenye maana katika kuwaokoa walioanguka. Vipengele vya mchakato vinadokeza jinsi ubinadamu na mahusiano ya kibinadamu yalivyo na thamani kwa Mungu. Kwa kuzingatia hili, shauku ya kukidhi matakwa ya taratibu za kanisa na sheria zinazohusiana na nidhamu haipaswi kuvuka lengo la jumuiya ya waumini kwa madhumuni yake ya kuwepo ya ukombozi.

 

 

NAFASI YA KWANZA YA KIBIBLIA

Mifano ya nidhamu, iwe iliyotolewa moja kwa moja na Mungu au na kikundi cha mtu mmoja-mmoja chini ya maagizo ya Mungu, imejaa katika Biblia. Dhambi za wana wa Haruni, Nadabu, na Abihu zilisababisha ghadhabu ya papo hapo ya Mungu (Law. 10). Yeroboamu mwana wa Nebati alipigwa kwa sababu ya uasi wake (2 Nya. 13). Dhambi za Yezebeli (2 Wafalme 9) zilisababisha hasira ya Mungu. Matukio mengine ukijumuisha kutotii kwa Uza (2 Sam. 6), amri ya wazi ya Mungu ya kuwaua manabii wa uongo (Kum. 13), unajisi wa Sabato (Neh. 13:15-22); uzinzi, na uasherati ambao ulisababisha adhabu ya kifo (Law. 20). Samsoni aliadhibiwa kwa ajili ya dhambi ya uasherati (Waamuzi 16) na Daudi aliadhibiwa na Mungu (2 Sam. 12:9, 10).

 

Wayahudi wa Agano Jipya walishughulika na nidhamu kama inavyothibitishwa na woga wa wazazi wa kipofu katika Yohana 9 ambao waliogopa kwamba wangeweza kutengwa nje ya sinagogi na viongozi wa Kiyahudi (fungu la 22). Kifo cha Anania na mkewe, Safira, kilichotokea kama matokeo ya kutotii kwa makusudi kanuni zilizowekwa za utoaji (Matendo 5), pia kinadokeza nidhamu ya kanisa. Mfano mwingine kutoka katika kitabu cha Matendo ya Mitume ni kuitwa kwa Stefano mbele ya baraza la Wayahudi, kitendo ambacho kilisababisha mauaji yake (Matendo 6; 7). Nyaraka za Paulo pia zinatoa ujuzi fulani katika nidhamu ya kanisa. 

 

Huenda inayotumika zaidi kati yao ni 1 Wakorintho 5:1-12, ambapo Paulo alikemea kanisa kwa uvumilivu wake kwa mshiriki ambaye alikuwa akijihusisha na uhusiano wa kimapenzi na mama yake wa kambo. Paulo aliagiza waziwazi kwamba mtu kama huyo aondolewe miongoni mwao. Akizungumzia kuhusu wale wanaochochea mapambano katika kanisa, mtume Paulo alipendekeza hatua za kinidhamu (Tito 3:10, 11; vifungu vingine vinavyohusiana na hivyo vinajumuisha 1 Tim. 1:19; 5:19-21; 2 The. 3:14, 15; Gal. 6:1; 2 Kor. 2:6-8).

 

 

UPENDO KAMA MSINGI

Kwa mujibu wa Mathayo, kuna hatua tatu za kutumia katika kuwaokoa waliokosea. Kwanza, mruhusu mkosaji ajue kwamba amefanya makosa (Mt. 18:15). Kama jitihada hii itashindwa kuleta matokeo yaliyotarajiwa, basi inalazimika kuleta shahidi mmoja au wawili (fungu la 16). 

 

Juhudi hizi za upatanisho zikishindwa tena, basi kanisa linapaswa kufahamishwa kuhusu jambo hilo (fungu la 17). Katika hatua hii, mkosaji anahatarisha hadhi yake katika jamii, anapohesabiwa kuwa “mtu wa mataifa” au “mtoza ushuru” kama hatasikiliza ushauri.

 

Wengine wanaweza kufikiria hatua hii ya tatu inasababisha kutengwa na kanisa, kuachwa, au aina nyingine ya kutengwa kijamii. Hata hivyo, hii haionekani kuwa kadhia, kwani mwenye dhambi hapaswi kudharauliwa au kupuuzwa bila kujali ukubwa wa kosa.3 Badala yake, awamu mpya ya malezi, kutunza, na kuweka katika hali nzuri kwa upande wa kanisa, imekuja yenyewe. Tunaona wazo kama hilo katika Waebrania 12:4-13, ambapo hatua za kurekebisha hufanya muunganiko kati ya nidhamu na upendo. 

 

Upendo kama msingi katika kusimamia nidhamu ni muhimu katika kutimiza lengo lake halisi. Akitilia mkazo zaidi msingi wa nidhamu, Paulo anasisitiza kwa kufaa kwamba wale ambao hawajaadhibiwa hawajapandikizwa ipasavyo katika familia ya Mungu, kwa maana ushahidi wa upendo wa Mungu kwa watoto Wake unaonyeshwa pia katika kuadhibiwa wanakokupata kutoka Kwake (fungu la 8). Hata hivyo, inastahili kufahamu kwamba sio nia ya Mungu kuwaweka watoto wake katika hali ya kudumu ya kutengwa na ushirika kamili wa kanisa, bali ni kuwahimiza wapate hali ya kiroho bora zaidi.

 

Wazo la kuanzisha jambo mbele ya shahidi zaidi ya mmoja (Mt. 18:16) linapatana na Kumbukumbu la Torati 19:15: “Shahidi mmoja asimwinukie mtu awaye yote kumshuhudia kwa uovu wo wote, wala kwa dhambi yo yote, katika makosa akosayo yo yote; jambo na lithibitishwe kwa vinywa vya mashahidi wawili, au watatu.” Ushuhuda wa mashahidi utamweka mshtakiwa (huru) au kumfanya mfungwa (kufungwa). Katika lugha ya Kiyunani Mathayo 18:18 inatafsiriwa kuwa “atakuwa amefungwa” na “atakuwa huru” na inatoa wazo la kuwa na uamuzi wowote wa kidunia unaoamuliwa au kuongozwa na uamuzi hapo juu.4 Kwa kudokeza, kuidhinishwa kwa uamuzi wa kanisa mbinguni unategemea utii wake kwa kanuni zilizowekwa katika Biblia –upendo, huruma, na utunzaji –katika namna ya kumtendea mkosaji.

 

 

UTUNZAJI BAADA YA ADHABU

“Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni” (fungu la 19)5. “Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina Langu, nami nipo papo hapo katikati yao” (fungu la 20). Maana ya muktadha wa kauli hii inaweza isiwe mbali na mashahidi wawili waliotajwa katika aya zilizotangulia (15, 16). Kwa hivyo, kukutana kwa wawili hao ni kutatua suala la mgogoro huo; kwa hiyo, usuluhishi unatazamiwa sana. Mfumo wa hukumu wa Kiyahudi unahitaji mashahidi wawili wawe wa kwanza kutekeleza hukumu ya mahakama (Kum. 17:7) na au kutoa “ombi la marufuku iliyotolewa wakati wa kutengwa na kanisa; au wangeweza kuwakilisha maombi kwa ajili ya toba na matokeo yake msamaha wa mtu aliyetengwa na kanisa.”6

 

Kwa kukataa shauri la kanisa yule mkosaji amejitenga na kundi la waumini na kushusha hadhi yake hadi katika kundi la “mtu wa mataifa na mtoza ushuru” (Mt. 18:17). Hii haimaanishi kwamba mkosaji anapaswa kupuuzwa, kwa vile wamataifa na watoza ushuru hawakuondolewa katika mpango wa wokovu, kama ilivyoonyeshwa na Yesu alipokabiliwa na kula na kushirikiana na wenye dhambi na watoza ushuru (Marko 2:13-17). Asili ya ujumuishi ya kazi ya wokovu inalazimu kuweka kila chombo mahali pake ili kuhakikisha juhudi ya kufikia kumrudisha mkosaji, kama vile inavyoweza kufanywa kwa wapagani au watoza ushuru ambao wana uhitaji mkubwa wa Mwokozi. Waumini wanapaswa kuwa waangalifu wasimpe mkosaji sababu moja ya kuhisi kana kwamba hakutendewa isivyo haki. 

 

Vivyo hivyo, washiriki wanahitaji kuwa waangalifu ili wasishiriki dhambi iwe kwa kushiriki au kwa kupuuza maovu kupitia aina yoyote ya huruma ya uongo baadaye.

NIDHAMU YA KANISA LA SIKU HIZI NA MATHAYO 18:15-20

Maandiko yameeleza dhahiri hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika mchakato wa kusimamia nidhamu. Kanuni muhimu zaidi ya matumizi ya Mathayo 18:15-20 katika kanisa la siku hizi kama inavyohusiana na mambo ya hatua za kinidhamu ni kwamba kuadabisha ni kwa ajili ya lengo la kumkomboa muumini aliyepotea. Siyo tu juu ya kukidhi matakwa ya sera ya kanisa kama ilivyoainishwa katika Mwongozo wa Kanisa, ambayo inaweza kuonyesha ulazima wa kuchukua hatua. Glenn Waddell anadai kwamba “kila hatua ya Mathayo 18:15-17 . . . lazima ichukuliwe kwa madhumuni na moyo unaoelekeza kukuza toba, upatanisho na kurudisha upya jamii ya agano.”7 Msimamo unaochukuliwa na wasiotubu “wa mataifa” au “watoza ushuru” unaliweka kanisa katika hali ya juu ya uwajibikaji katika kuhakikisha wokovu wa mshiriki aliyepotea kama walivyoweza kwa mpagani ambaye kwa sababu yake kanisa lipo. 

 

Akizungumza katika mwelekeo huu, Wyman L. Richardson anadai kwamba “Ilikuwa hata hivyo, kwa ajili ya Mataifa na watoza ushuru, watu wasiostahili, tumaini la injili lilitolewa katika Kristo. Kwa hivyo sasa tunapaswa kumtendea ndugu yetu aliyeanguka kama ambavyo mmishonari angemtendea mtu ambaye hajasikia injili. Tunapaswa kuwahubiria injili, kuwaeleza upya tena maana ya kuwa Mkristo, na kuwasihi warejee.”8

 

 

FAIDA ZA NIDHAMU YA KANISA

Kuna faida ya hatua za kinidhamu zinapofanywa kwa usimamizi wa Roho Mtakatifu. Katika matukio fulani washiriki waliokosea na kuadibishwa huthamini uingiliaji kati wanapoelewa kwamba ulikuwa kwa ajili ya kuwasaidia kiroho. Nidhamu humpa mkosaji fursa ya kujikita zaidi katika imani anapojifunza mafundisho na maelekezo ya dini kwa uzito zaidi. Zaidi ya hayo, hatua za kinidhamu husaidia kuwazuia wengine kutokufuata mfano wa tabia mbaya. Hii inasaidia kulinda jamii ya waumini. Kama vile Paulo alivyomwonya Timotheo: “Wale wadumuo kutenda dhambi uwakemee mbele ya wote, ili na wengine waogope” (1 Tim. 5:20).

 

Nidhamu ya kanisa inatoa fursa kwa kanisa kupata uhusiano bora na thabiti zaidi kwa Kristo na mtu mwingine. “Mkatoe ile chachu ya kale” Paulo anaandika, “mpate kuwa donge jipya” (1 Kor. 5:7). Nidhamu inaposimamiwa kwa upendo na kufuata mwongozo uliowekwa katika Maandiko, ina uwezo wa kudumisha uaminifu wa kiroho na maadili ya kanisa. Ellen White anasisitiza kwamba “basi uovu unapaswa uonekane jinsi ulivyo, na lazima uondolewe ili usizidi kuenea zaidi na zaidi.”9 Zaidi ya hayo, nidhamu ya kanisa huongeza ukuaji wa kiroho wa kanisa na ustawi wake.10 Wokovu wa mwenye dhambi kutoka katika nguvu za dhambi na matunda yake ndio kiini cha mpango wa wokovu kwa wanadamu (Kol. 1:12, 13).

 

 

HITIMISHO

Kanisa ni njia ya thamani sana ya kurahisisha wokovu wa watu. Hatua za kinidhamu ni hatua za kusahihisha ambazo zinapaswa kutoa mazingira ya wokovu kwa wakosaji. Sambamba na hilo, nidhamu ya kanisa husaidia kudumisha kiwango cha juu cha kuchukia dhambi ambacho kina mwelekeo wa kuleta lawama kwa kazi ya Mungu na kwa hivyo kuhafifisha jina lake “Nuru ya Ulimwengu.” Kila mwanajamii ana wajibu mkubwa wa kutafuta njia ya kuwasaidia wakosaji ili kurejea hatua zao hadi kwenye uhusiano unaookoa na Mungu kama wataradhia wa kwenda mbinguni. Ni jukumu la kanisa kuweka utaratibu fulani wa kutoa tumaini kwa waliopotea pamoja na njia za kuwasaidia kushinda mielekeo yao ya dhambi.

Mnamo mwaka 1850 Stephen Smith, wa Unity, New Hampshire, alikuwa akiingia katika nyanja ya huduma kwa umma lakini aliangushwa na mafundisho yenye makosa. Alikataa kukubaliana na mashauri ya maonyo, akapata mawazo mengine ya ajabu, na kujiunga na upinzani. Kwenye kongamano kule Medford, Massachusetts, James na Ellen White walikabiliana na kazi yake.

 

James aliandika: “Tulipowasili pale, utengano ulikuwepo miongoni mwa ndugu. Walikuwa wametembelewa na Stephen Smith na Josiah Hart, ambao walikuwa wamejaribu kuwajengea chuki dhidi yetu. Hilo lilikuwa na athari mbaya lakini tuliendelea na mkutano.

 

“Jukumu la mkutano ule lilikuwa kuweka bayana makosa ya Stephen Smith, H. W. Allen, na umuhimu wa kanisa kuchukua hatua dhidi mwelekeo wa baadhi ya ndugu. Ellen alipata njozi ambapo aliona kuwa Mungu alikuwa amechukizwa nasi kama jamii ya watu Wake, kwa kuwa kitu kilicholaaniwa kilikuwa kambini, yaani, mafundisho ya makosa miongoni mwetu, na kwamba kanisa lazima lichukue hatua, na njia pekee ya kuwasaidia Ndugu Allen na Smith ilikuwa ni kuwaondolea ushirika wa kanisa, kutokana na msimamo wao wa sasa. Wote walitendea kazi nuru waliyopewa, wote walipokea njozi, na hata kwa mtu mmoja mmoja, wote waliinua mikono kuwaondoa katika ushirika wa kanisa.”

 

 

KONGAMANO LA WASHINGTON, NEW HAMPSHIRE
Ellen White aliuelezea mkutano wa Washington (1851) kwa kina, akitoa mitazamo inayoangazia kile kilichotokea.

 

“Kule Washington Bwana aliongoza mkutano Yeye Mwenyewe. Stephen Smith na E.P. Butler pamoja na watu 75 walikuwepo, wote wakiwa na imani moja. Stephen Smith alikuwa amejazwa na roho potovu. J. Hart pamoja naye walikuwa wamejaza mawazo ya wengi kwa chuki dhidi yetu, taarifa za uongo zilikuwa zimeenezwa. Kundi lilikuwa likizama na kupoteza nguvu ya ujumbe wa malaika wa tatu. Walikuwa dhaifu lakini hawakujua sababu lakini sababu ilikuwa kwamba kulikuwa na kitu kilicholaaniwa katika kambi na kwa msaada wa Mungu tulikuwa tunajaribu kukitoa ndani ya kambi.”

 

“[Siku ya Sabato] nilichukuliwa katika njozi. . . . Hali ya mambo kule Washington ilifunuliwa kwangu, ambayo niliieleza wazi kwao. Njozi ilikuwa na matokeo makubwa. Wote walikiri kuziamini njozi zile isipokuwa ndugu Butler na Stephen Smith. Sote tulijisikia kuwajibika kuchukua hatua, na kwa kura ya ndugu ya pamoja, Smith aliondolewa katika ushirika wa kanisa hadi pale atakapoachana na mitazamo yake potovu.”

 

Yapata mwaka mmoja tangu aondolewe katika ushirika, Smith alianza kuona makosa yake, akakiri na kurejeshwa katika ushirika wa kanisa (1852). Hili liliendelea kwa miezi michache, kisha kwa mara nyingine tena akajihusisha katika mitazamo potovu naye akaondolewa katika ushirika. Mwaka 1857 akarejea tena, ila kwa kitambo tu.

 

Wakati fulani mnamo miaka ya 1850 baada ya moja ya kuteleza kwake, Ellen White alimwandikia ushuhuda ambapo alionyesha jinsi ambavyo maisha yake yangekuwa kama angeng’ang’ania mwelekeo aliokuwa akiufuata. Alipopokea ile barua, aliogopa kwamba ulikuwa ushuhuda wa makemeo, hivyo akaenda nayo nyumbani kutoka posta akaitupa ndani kwenye sanduku bila kuifungua na kuisoma.


Kwa karibia miaka 30 Smith alikuwa nje ya kanisa, akiwapinga waliowahi kuwa ndugu zake, akiwa mwenye hila na mwenye kuumiza katika ukosoaji wake. Mke wa Smith alibakia mwaminifu, na gazeti la Review la kila juma lililetwa nyumbani kwao. Siku moja Smith alilichukua na kusoma makala iliyoandikwa na Ellen White. Aliendelea kusoma makala zake na kuona kuwa zinagusa moyo wake na moyo wake ukaanza kulainika.

UAMSHO NA MATENGENEZO

Mnamo mwaka 1885, E. W. Farnsworth alikuwa akiendesha uamsho katika kanisa la Washington. Smith alitembea umbali wa maili 12 kuhudhuria mikutano ya Sabato. Hubiri lilipoisha Smith akasimama na kuomba kuzungumza. Mkutano ulitarajia ukosoaji na maneno ya hila.

 

“Sitaki mniogope, ndugu zangu,” alisema. “Sikuja kuwakosoa. Nimeachana na mambo hayo.” Kisha akazungumzia alivyofanya hapo awali, chuki yake kwa mfumo wa kanisa, kujiunga na vikundi vya upinzani kimoja baada ya kingine, ambavyo alikuwa ameshuhudia vikianguka na wafuasi wake wakiishia kuchanganyikiwa. “Kweli” alisema, “ni vitu visivyobadilika, lakini kweli ni kwamba wale ambao wameipinga kazi hii wameishia kuharibikiwa, wakati ambapo wale ambao wameendelea kuiunga mkono wamestawi, wameendelea kuwa bora, waliojitoa zaidi, na wacha Mungu. Wale walioipinga wameishia kujifunza kupigana na kufanya midahalo. Wamepoteza dini yao yote.


“Hakuna mtu mkweli atakayeshindwa kuona kuwa Mungu yuko nao na yu kinyume chetu. Nataka kuwa katika ushirika na watu hawa kwa dhati ya moyo na kanisani.”

 

Stephen Smith alikumbuka barua kutoka kwa Ellen White aliyoitupa kwenye sanduku nyumbani kwake. Alipofika nyumbani kwake, punde alikuwa na bahasha iliyofungwa mikononi mwake.  Akaifungua na kuisoma. Alirejea Washington ambapo alimsikia Farnsworth akihubiri juu ya Roho ya Unabii. Hubiri lilipoisha alisimama tena. 

“Nilipokea ushuhuda mimi mwenyewe miaka 28 iliyopita. Niliupeleka nyumbani na kuuweka sandukuni na sikuwahi kuusoma hadi Alhamisi iliyopita.” Alisema hakuwa ameuamini ushuhuda huo hata kama hakuusoma. Aliogopa kuusoma, akihofia kuwa ungemkasirisha. Lakini, akasema, “karibia muda wote nilikuwa na hasira.”


“Ndugu zangu, kila neno la ushuhuda kwa ajili yangu ni kweli, na ninaukubali. Nimefikia pale ambapo hatimaye ninaamini kuwa [shuhuda] zote ni za Mungu, na kama ningezingatia ule ambao Mungu aliutuma kwangu hali kadhalika na zingine zote, ungekuwa umebadilisha mwelekeo wote wa maisha yangu, na ningekuwa mtu tofauti kabisa.”

 

“Mtu yeyote ambaye anasema kweli lazima aseme kwamba zinamwelekeza mtu kwa Mungu na Biblia wakati wote. Kama ni mkweli, atasema hivyo; kama hatasema hivyo hasemi kwa dhati ya moyo wake. Kama ningekuwa nimezizingatia, zingekuwa zimeniokoa na ulimwengu wa shida. . . . Nilidhani nilikuwa na ujuzi kama wa ‘njozi za mwanamke mzee’ kama nilivyokuwa nikimwita. Naomba Mungu anisamehe! Lakini kinachonihuzunisha ni kugundua kuwa njozi zilikuwa sahihi, na mtu yule aliyedhani kuwa alijua kila kitu alikuwa amekosea. Shuhuda ziko sahihi nami nimekosea.”


“Ndugu zangu, mimi ni mzee kiasi cha kutoweza kufuta yote niliyokosea. Mimi ni dhaifu kiasi cha kutoweza kufika kwenye mikutano yetu mikubwa, lakini nataka muwaambie watu wetu kila mahali kuwa mwasi mwingine amejisalimisha.”

 

Badiliko halisi, lilitokea katika maisha na uzoefu wa Stephen Smith, na alikumbukwa katika maisha yake ya baadaye kama Mwadventista aliyejitoa kikamilifu mwema na mwenye huruma.

Katika kanisa moja nililokuwa mchungaji mwanzoni katika huduma yangu, nilikutana na mhandisi mwenye elimu, mwenye uhusiano mzuri na watu, kutoka katika familia tajiri sana. Inavyoonekana, wachungaji walionitangulia hawakuwahi kushughulikia suala lililomhusu mtu huyu ambalo kila mtu kanisani alilijua. Kwa kweli hawakupata njia sahihi ya kulishughulikia. Suala lilihusu utunzaji wa Sabato–mtu huyu alikuwa akifanya kazi siku ya Sabato. Alikuja kanisani wakati wowote alipoweza, lakini Sabato nyingi, alikuwa akifanya kazi. Na kanisa lililijua hilo.

 

Kulikuwa na baadhi ya watu kanisani waliosema, “Tunapaswa kufanya jambo juu ya hili. Mtu huyu anavunja Sabato. Tunawezaje kuwaambia watu kufuata sheria wakati tunamruhusu mtu huyu kuvunja sheria, na hakuna kitu ambacho kimefanyika kwa miaka mingi?” Kisha, kulikuwa na wale ambao walihisi tofauti juu yake. “Bado ni kijana,” walitoa hoja. “Mbali na hilo, ni mtu mwaminifu sana kwa kanisa katika zaka na sadaka,” wangeongeza. Pasipo kusema, ilikuwa ikisababisha shida kanisani.

 

 

KUCHUKUA HATUA

Nilipoingia kama mchungaji, nilisikia kutoka pande zote mbili na ikabidi nijiulize swali, “Nifanye nini? Jukumu langu ni lipi?” Niliposoma Biblia, Roho ya Unabii, na Mwongozo wa Kanisa, nilitambua kwamba ninapaswa kufanya jambo fulani. Sio kwa sababu ya wale waliotaka nimfute ushirika au kumleta kanisani kwa ajili ya nidhamu, lakini kama nilipaswa kufanya jambo fulani lilipaswa kuwa msaada kwake. Hiyo ndiyo njia niliyoichagua. Siyo kumhukumu mtu huyu, kwa vitisho vya matokeo ikiwa asingerudi kwenye mstari, jambo ambalo kundi moja kanisani lilikuwa likinisukuma kufanya. Walikuwa wamewashinikiza wachungaji waliotangulia hadi wachungaji wakaamua kutogusia suala hilo. Hilo halikuwa chaguo kwangu.

 

Kwanza, nilianza kumwombea. Baada ya muda, nilimwambia nilitaka kumtembelea nyumbani kwake. Alikuwa na woga kidogo kwa sababu alikisia sababu iliyonifanya nimtembelee. Hatimaye, hata hivyo, alikubali. Katika safari yangu ya kwanza hata sikuzungumza kuhusu Sabato. Nilifanya tu mazungumzo ya kirafiki pamoja naye, nikaomba naye, kisha nikaondoka. Alifurahi sana kwa sababu alikuwa akijiandaa kwa makabiliano. Katika safari yangu iliyofuata, tulizungumza, nikaomba naye, na sikusema chochote kuhusu hali yake na Sabato. Hata hivyo, tulizungumza kuhusu maisha yake ya kiroho na umuhimu wa kukua kiroho. Pia tulizungumza kuhusu umuhimu wa sheria ya Mungu. Nilipoendelea kumtembelea, tulianzisha utaratibu wa kutembelea.

 

Hatimaye, katika mojawapo ya safari zetu, nilileta mada ya Sabato. “Unajua,” akajibu, “nimekuwa nikifanya hivyo kwa miaka mingi, na wachungaji wengi wamepita hapa na hawajawahi kuongea na mimi kuhusu jambo hili.” Ni dhahiri kwamba kampuni aliyoifanyia kazi ilikuwa imelikataa ombi lake la kuiondoa Sabato katika ziku za kazi. “Walisema, hapana. Hawawezi kunipa upendeleo huo kwa sababu wakinipa, basi wanapaswa kuwapa watu wengine pia.”  “Uko tayari kujaribu tena?” Niliuliza. “Hebu tuliombee hili jambo,” nilisihi. “Siyo juu ya kile ninachotaka. Ni kuhusu kile Mungu anachotaka kwa ajili ya maisha yako. Siyo juu ya kanisa kukuambia unachopaswa kufanya. Ni kuhusu wewe kuweza kuja kanisani siku ya Sabato kumwabudu Mungu.” “Hapana,” alisisitiza, “sijali sana juu ya hilo. Sitaki kujaribu tena.”

 

Wakati huo, nilimjulisha kwamba nililazimika kuzungumza jambo hilo kanisani. Kanisa lingeamua cha kufanya juu ya suala lake. “Huwezi kunifanya chochote!” Alisema kwa dharau. Nilimhakikishia kwamba nilitaka tu kumsaidia yeye na familia yake. Kuileta ili ishughulikiwe na kanisa ilikuwa hatua iliyofuata. Baada ya kuomba naye, niliondoka.

WAKATI MWINGINE INASAIDIA

Sabato iliyofuata, alikuja kanisani. Kumbuka, alikuja kanisani mara moja tu kwa mwezi au zaidi kabla ya hapo. Sabato hiyo, alikuja na kuomba kuzungumza nami faraghani. “Nataka kukushukuru,” alianza, “kwa kunisaidia kuona kile ambacho nilikuwa sikioni. Kwa miaka mingi, nimekuwa nikivunja sheria, nikijua kwamba nilikuwa nikifanya jambo lisilo sahihi. Ingawa nilijihisi kuwa na hatia juu ya hilo, hakuna mtu aliyewahi kuzungumza nami jinsi ulivyofanya, kwa hiyo nilikukasirikia! Lakini sasa ninatambua kwamba ulikuwa unajaribu kunisaidia tu kiroho na ninataka kukushukuru kwa hilo.”

 

Kuanzia siku hiyo na kuendelea, alikuja kanisani kwa shauku kila Sabato. Hata alishiriki na washiriki wengine wa kanisa jinsi alivyofurahishwa kwamba tuliweza kuzungumza mambo na kutatua suala hilo bila kulikuza hadi kwenye baraza la kanisa.

 

Uzoefu wangu ulinifundisha kwamba hatua zinaweza kuchukuliwa ili kumsaidia ndugu au dada aliyekosea kabla ya kufikia hatua ya nidhamu ya kanisa. Ninaziita hatua za upendo, ambapo unampenda mtu huyo kweli kweli, unaomba kwa ajili yake, unamtembelea, unajifunza Biblia pamoja naye, na kumjali. Unapofanya hivyo, huenda usilazimike kwenda zaidi kiasi cha hatua za kinidhamu za kanisa. Je, inasaidia wakati wote? Hapana, si kila wakati inasaidia. Kunaweza kuwa na baadhi ya watu wanaosema, “Hapana! Sahau hilo.” Lakini wakati mwingine inasaidia. Na ni njia sahihi ya kufanya hivyo kwa sababu kuadhibu ni juu ya kuwakomboa watu. Siyo juu ya kuwaadhibu watu kwa makosa yao. Ni juu ya kuwaita warudi kwenye uhusiano sahihi na Yesu. Na wanapotii wito huo, mbingu hufurahi, na watu hufurahi. Kuna wakati kanisa liliwaadhibu watu kwa kila kosa dogo. Leo, tuna uwezekano mkubwa wa kuruhusu kila kitu kiende. Lakini tunapaswa kuwa waaminifu kwa watu. Kuepuka mambo hakusaidii chochote. Ndiyo, kanisa ni jumuiya ya watu waliovunjika. Sisi sote tuna changamoto zetu; sote tuna aina zetu za udhaifu. 

 

Tunakusanyika pamoja kama kanisa kuunda familia katika Kristo, kila moja ikileta udhaifu kwetu ambao unahitaji uponyaji. Kwa hivyo tunahitaji uongozi unaojua na kuelewa neema kutoka katika uzoefu binafsi ili kusimamia neema, upendo, na msamaha kwa washiriki waliokosea. Je, siyo vizuri kujaribu kumsaidia mtu kwa upendo kuliko kumwacha aendelee kushuka katika njia iendayo kwenye uharibifu?

Utume wetu, ushirikiano huu mkuu tulio nao na Mungu katika kutangaza ujumbe wa malaika watatu ulimwenguni, unanufaika kutokana na muundo na utaratibu. Sote tunapouridhia, muundo wa Kanisa la Waadventista wa Sabato unatoa mfumo wa kuongoza uenezaji wa injili wenye ufanisi. Hata hivyo, kuna nyakati, ambazo utaratibu haufungamani na makubaliano yaliyofikiwa na wawakilishi wengi wa kanisa. Asili ya makubaliano yanayoshikiliwa na utaratibu wa kanisa la Waadventista wa Sabato na njia ambazo umoja unaweza ukapatikana ndiyo mada ya makala hii.

 

 

MUHIMU

Nidhamu ya kanisa, kwanza kabisa, haitokani na kanisa. Inatoka kwa Mungu. Amri Kumi, udhihirisho halisi wa tabia ya Mungu ya upendo, zinaeleza jinsi tunavyopaswa kuhusiana na Mungu na watu wengine. Kama wenye dhambi, tumeivunja sheria kamilifu ya Mungu ya upendo lakini tunapokubali wokovu wake, Mungu hutuhesabia haki pasipo kustahili kwetu. Kisha utakaso unakuja, kwani tunapaswa kufanana Naye zaidi na zaidi, yote kwa uwezo Wake. Mchakato huo unahitaji hatua za nidhamu za rehema ili kutuleta katika uhusiano bora na Bwana anapotafuta kurejesha sura yake ndani yetu. Basi, nidhamu, ni sehemu muhimu ya mpango wa wokovu. Ni njia ya kutuleta karibu zaidi na Bwana.

 

Mika 6:8 inatoa mhimili wa nidhamu ya kanisa. Inatuambia kwamba Mungu ametuonyesha kile kinachotarajiwa kutoka kwetu, nacho ni, kwanza, kufanya kile ambacho ni sahihi na haki. Tunahitaji heshima na upendo kwa amri za Mungu na kufanya mambo katika njia inayostahili. Ingawa tunaelewa kwamba tunapaswa kufanya yaliyo sahihi, si kila mara tunafanya hivyo. Kwa hiyo jambo la pili la Mika ni kwamba tunapaswa kupenda rehema. Kuwa mwenye rehema ni sehemu nyingine ya nidhamu inayokusudiwa kutuvuta karibu zaidi na Mungu katika uhusiano wenye upendo. 

 

Mungu hatukatai kwa sababu hatufanyi yaliyo sahihi. Analeta rehema kwa ajili yetu. Tunapaswa pia kufuata mfano wake. Hii haimaanishi kutoa udhuru kwa dhambi. Inamaanisha kwamba tunalenga katika upatanisho wa kurudi tena kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu. Sehemu ya mwisho ya kanuni ya nidhamu ya Mika inatuambia kwamba tunahitaji kutembea kwa unyenyekevu pamoja na Mungu wetu, tukitia kila jitihada za nidhamu katika mwongozo Wake wa hekima.

 

Kanisa halikuanzisha hatua mpya za kinidhamu kwa sababu lilitaka tu. “Biblia na Roho ya Unabii vimeweka wazi, kwa lugha dhahiri wajibu mzito ambao uko juu ya watu wa Mungu kudumisha usafi wao, uadilifu, na juhudi za kiroho. Kama washiriki wakikosa kujali au kutanga mbali, kanisa lazima litafute kuwarejesha kwa ajili ya Bwana.”1 Dhana ya nidhamu ya kanisa inahusiana na hitimisho la urejeshwaji wa wanadamu katika sura ya Mungu.

 

Katika siku za awali kabisa za kuwepo kwa madhehebu yetu, kabla hata ya kuwa na Konferensi Kuu iliyoratibiwa vema, watu hawakutaka kukubali aina yoyote ya fundisho ambalo lingewalazimisha watu kuamini katika imani fulani. Kila kitu kiliachwa kwa mtu binafsi. Hawakutaka kanuni za imani nje ya Biblia nzima. Hata hivyo, kanisa lilipoendelea kukua, hitaji la utaratibu liliongezeka na ikawa wazi, kanisa la Waadventista wa Sabato lilipoanzishwa, kwamba namna fulani ya kanuni na michakato vingewezesha utendaji mzuri wa kanisa.

 

 

MAKUBALIANO

Ngazi za kiutawala za kanisa hutoa miongozo, na katika baadhi ya matukio kanuni, za jinsi tunavyopaswa kutenda, kuhusiana, na kuwa sehemu ya watu wa Mungu waliosalia wa siku za mwisho. Miongozo na kanuni hizi zimewekwa katika sera ya kanisa ambayo hupitishwa katika mikutano iliyoteuliwa. Mwongozo wa Kanisa ni wa muhimu sana kwamba, ingawa mabadiliko yanaweza kupitishwa kama mapendekezo katika Vikao vya Mwisho wa Mwaka au vya Kamati Tendaji, baada ya hapo ni lazima yatumwe kwenye Sesheni ya Konferensi Kuu ili kupitishwa. Mwongozo wa Kanisa unashughulikia hasa nidhamu ya kanisa katika muktadha wa kanisa mahalia. Hata hivyo, mtu anaweza kuona, jinsi inavyohusiana pia na konferensi mahalia, union, divisheni ya Konferensi Kuu, na Konferensi Kuu inayowakilisha eneo la ulimwengu kwa vile kila mwajiriwa wa kanisa ni mshiriki wa kanisa mahalia.

 

Mtu ambaye amempokea Yesu Kristo kama Mwokozi wake binafsi anapokuwa mshiriki wa Kanisa la Waadventista wa Sabato, anakubali mfumo wa imani wa Kanisa na kuapa kuishi kulingana nao. Ikiwa utafika wakati ambapo haamini tena kama jinsi Waadventista wanavyoamini au kuchagua kutokuishi jinsi Waadventista walivyojitoa kuishi, anakanusha kujitoa kwake hapo awali kuwa mshiriki wa kanisa. Ushirika katika Kanisa la Waadventista wa Sabato unashikiliwa kwa ukubali wa wale walio katika kanisa mahalia.

 

Kadhalika, kwa mfumo wa kiutawala, Kanisa la Waadventista wa Sabato hufanya kazi kwa makubaliano ya pande mbili. Ni kupitia kwa makubaliano haya, sera za kazi za Kanisa zinaundwa. Haya ni makubaliano ya pande mbili kuhusu jinsi tutakavyotekeleza utume wa kanisa bila kuingiliana na kushindana kati ya mtu na mwingine. Mambo hayo siyo Biblia, lakini yanatokana na kanuni za kibiblia za jinsi tunavyoweza kufanya kazi kwa upatanifu chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu ili kutimiza utume Wake. Kumbuka kwamba kusudi kuu la Kanisa la Waadventista wa Sabato si tu kuwa na mfumo unaofanya kazi vizuri, na kujaribu kuwahudumia washiriki wake, na kuisaidia jamii. Kwa hakika hiyo ni sehemu yake. Lakini kusudi kuu la Kanisa la Waadventista wa Sabato ni kutangaza Ujumbe wa Malaika Watatu wa Bwana na kuwatayarisha watu kwa ajili ya ujio wa Yesu uliokaribia.

 

Mamlaka ya nyaraka za sera zilizoundwa na kanisa yamejengwa kwenye muundo wa utawala wetu, ambao “uko katika utaratibu wa uwakilishi ambapo mamlaka na wajibu wa kiutendaji vimewekwa katika ngazi mbalimbali za kiutawala na taasisi pamoja na maeneo yake ya uchaguzi, bodi zake, au maofisa wake kupitia katiba au ibara za ujumuishaji, sheria ndogo ndogo, na sera na miongozo ya uendeshaji.”2 

 

Ukweli kwamba uongozi wetu ni uwakilishi unamaanisha kuwa sauti za ulimwengu mzima zinawakilishwa katika maamuzi ya sera. Vipengele vyote vya Kanisa vinahusika katika kuamua sera zitakavyokuwa na hivyo kukubali kutii sera.

 

Vyombo vya utawala haviwezi kuamua tu kufanya chochote wanachotaka, pasipo kudhoofisha uadilifu wa kimuundo wa kanisa. Tumeunganishwa pamoja kupitia kwa makubaliano ya kiutawala kuwa sehemu ya familia ya Waadventista. “Hadhi ya kiutawala inatolewa kwa eneo la kiutawala kama amana. 

 

Kutambuliwa rasmi . . . sio kujipatia wenyewe, au kuja yenyewe tu moja kwa moja, au ya kudumu. Ni matokeo ya uamuzi rasmi wa kamati tendaji au kikao cha kiutawala katika ngazi za juu za utawala wa madhehebu. Ushiriki na hadhi ya utawala hukabidhiwa kwa vyombo vinavyokidhi sifa fulani ikiwa ni pamoja na uaminifu kwa Imani za Msingi za Waadventista wa Sabato, kufuata desturi na sera za madhehebu, udhihirisho wa uwezo wa kutosha wa uongozi na fedha, na mwitikio kwa changamoto na fursa za utume. Ushiriki na hadhi vinaweza kupitiwa, kusahihishwa, kurekebishwa, au kuondolewa na ngazi ya uongozi iliyouidhinisha.”3

 

“Ufanyaji wa maamuzi unatokana na michakato ya pamoja inayoruhusu ushiriki wa wajumbe.” Mtu mmoja, hata kama angekuwa rais/mwenyekiti wa shirika, hawezi kutoa amri za sera au kuamua hadhi ya shirika/taasisi. 

 

“Mamlaka ya juu kabisa ndani ya uwezo ulioidhinishwa kwa kila ngazi ya kiutawala wa madhehebu inakuwa kwenye kikao cha jimbo.”4 Maamuzi yoyote yanayofanywa, au hatua zinazochukuliwa na chombo cha kiutawala zinaweza kupitiwa tena au kutenguliwa na jimbo lake. Zaidi sana, uamuzi wowote wa jimbo au wa kamati tendaji unaweza kupitiwa na chombo cha ngazi ya juu. “Inapotokea tofauti ndani au kati ya vyombo mbalimbali vya utawala na taasisi juu ya mada ambazo hazijafafanuliwa bado kwenye Katiba na Sheria, katika Sera ya Kazi ya Konferensi Kuu, au katika maamuzi ya Kamati tendaji ya Konferensi Kuu kwenye kikao cha Mwaka, ni sahihi kukata rufaa kwenda ngazi ya juu zaidi ya utawala ambayo haikujihusisha moja kwa moja kwenye suala hilo.”5 Ngazi ya juu zaidi ya mamlaka ya kiutawala ikiwa ni Sesheni ya Konferensi Kuu, ambayo ina mamlaka juu ya ngazi zingine zote.

 

Katiba na Sheria za Konferensi Kuu, tamko la utume na sera zilizokusanywa au zilizorekebishwa zilizopitishwa na Vikao vya Konferensi Kuu na Vikao vya Mwaka vya Kamati Tendaji ya Konferensi Kuu zinaweza kupatikana katika Sera ya Kazi ya Konferensi Kuu. “Kwa hiyo, ndiyo sauti yenye mamlaka ya Kanisa katika mambo yote yanayohusu utume na usimamizi wa kazi ya madhehebu ya Waadventista wa Sabato katika sehemu zote ulimwenguni.”6 Ni kweli, sio Maandiko Matakatifu, bali Sera ya Kazi ndiyo ambayo mifumo yote ya utawala ya Waadventista wa Sabato imekubali kuitii kupitia utawala wa kiuwakilishi wa mfumo wetu. Ingawa mambo ya kutokubaliana katika suala la sera yanaweza kutokea, muundo wetu ni kwamba tutii maamuzi yanayotolewa na chombo cha maamuzi husika kinachotuwakilisha.

 

Kuzingatia kikamilifu Sera ya Kazi ya Konferensi Kuu husaidia kudumisha umoja wa Kanisa. Kama kutoka nje ya sera ni lazima, vyombo vyetu vya utawala vinapaswa kuomba idhini ya awali kutoka kwa Kamati Tendaji ya Konferensi Kuu. “Inapotokea sheria/mabadiliko ya sheria zinazoongoza nchi zinaonekana kukinzana na sera za madhehebu ni uvunjifu wa sheria, mfumo utachukua hatua kwa mujibu wa sheria, kwa masharti yafuatayo: 

 

a. Ushauri umetafutwa kutoka kwa maofisa wa Konferensi Kuu (mwenyekiti, katibu, na mhazini/afisa mkuu wa fedha) na imethibitishwa kwamba sera za madhehebu hakika zinakiuka sheria. 

 

b. Utiifu wa sheria haujumuishi ukiukaji wa kanuni za maandiko.”7

 

Watendakazi wa shirika katika uongozi wa utendaji wanapaswa kuwajibika kwa vyombo vyao vya uongozi. “Maofisa na viongozi wanatarajiwa kufanya kazi kulingana na Sera ya Kazi ya Konferensi Kuu. Wale wanaoonyesha kutokuwa na uwezo au kutokuwa tayari kusimamia kazi zao kwa kufuata sera wasiendelezwe katika uongozi wa kiutendaji na majimbo yao au bodi/kamati za uongozi.”8

WITO

Ellen White anaandika “Mara nyingi nimeagizwa na Bwana kwamba hakuna uamuzi wa mtu yeyote unaopaswa kuwekwa katika uamuzi wa mtu mwingine yeyote.” Bwana anaheshimu haki ya watu kutoa mawazo yao wenyewe, kwa hivyo hatupaswi kuwalazimisha watu pia. “Wala mawazo ya mtu mmoja au mawazo ya watu wachache,” anaendelea, “yasichukuliwe kamwe kuwa ya kutosha katika hekima na uwezo wa kuongoza kazi na kusema mipango inayopasa kufuata. Lakini, wakati wa katika Konferensi Kuu, maamuzi ya ndugu waliokusanyika kutoka sehemu zote za maeneo ya kazi yanapotumika, uhuru binafsi na uamuzi binafsi haupaswi kudumishwa kwa ushupavu, bali usalimishwe. Kamwe mtendakazi asichukulie kama sifa njema kuendelea kushikilia msimamo kwa nafasi yake ya uhuru, kinyume na uamuzi wa jumuia nzima ya waumini.”9

 

Kutembea kwa unyenyekevu mbele za Mungu ni kukubali ukweli kwamba akili ya mtu mmoja au mawazo ya wachache hayatoshi katika hekima. Tuna nguvu tukiwa pamoja. Ndiyo maana tunaamua sera na vipengele vya Mwongozo wa Kanisa kama kundi kubwa la watu. Roho Mtakatifu anafanya kazi kupitia uongozi wa kundi zima pamoja, kama Maandiko yanavyotuambia, “Bali kwa wingi wa washauri huja wokovu” (Mit. 11:14).

 

Tunapaswa kujinyenyekeza wenyewe kwanza kwa Bwana, na baadaye kwa jumuia ya waumini, na kutambua kwamba tunaweza tusiwe na majibu yote sisi wenyewe. Tunaweza kumwomba Bwana atusaidie kuelewa vyema jinsi ya kuhusiana na jambo lolote fulani ambalo hatukubaliani nalo, na Bwana atatuongoza katika ukweli wote na kutuunganisha. Baadhi ya watu huchanganya umoja na ulinganifu. Umoja haumaanishi kwamba kila mtu anapaswa kuamini kuwa rangi ya samawati ndiyo bora zaidi. Inamaanisha tu kwamba mioyo yetu itaunganishwa katika lengo, pasipo hasira au chuki dhidi ya wale wanaopendelea zulia la kijani dhidi ya zulia la samawati kwa ajili ya kanisa lao.

 

Mojawapo ya njia bora za kufikia umoja na upatanifu ni kuzingatia uhusiano wetu binafsi na Yesu pamoja na utume Wake kwa kanisa. Ellen White anaandika, “Ndugu zangu, msiruhusu kitu chochote kiingie kitakachowatenganisha ninyi au na Mungu. Msizungumze juu ya tofauti za mawazo yenu, bali muungane katika upendo wa ukweli kama ulivyo katika Yesu. Njooni mbele za Mungu, na omba damu iliyomwagwa ya Mwokozi kama sababu ya ninyi kupaswa kupokea msaada katika vita dhidi ya uovu. Hutaomba bure.10 Tunapaswa kuelewa kwamba mengi yanayohusika na nidhamu yanahusiana na uhusiano wetu binafsi na Bwana na jinsi gani tuko tayari kujinyenyekeza kwa yale ambayo Mungu anataka na kwa yale ambayo ameonyesha kupitia mfumo wake katika muundo wa uwakilishi.

 

Kama mfumo wa kanisa umepitisha sera fulani, lakini mfumo haufanyi kazi kulingana na sera iliyopitishwa, inaleta hali yenye changamoto. Mchakato wetu wa katiba, sera, na desturi zina dhana moja ya msingi: kwamba wote tumebadilishwa. Kwamba, hata hivyo, inaweza isiwe kweli kwa watu wote, wakati wote, na katika ngazi zote za utawala. Hapa ndipo penye tatizo. Kama sisi wote tungebadilishwa na kuunganishwa na Kristo, uvunjifu huo usingetokea kamwe, na kama ungetokea, tungetubu kwa ufahamu wetu juu yake. “Kama kiburi na ubinafsi vingewekwa kando,” Ellen White anaandika, “dakika tano zingeondoa matatizo mengi sana.”11

 

Iwe katika kanisa mahalia, katika Konferensi, Union, Divisheni, au Katika kikao cha Kamati Tendaji ya Konferensi Kuu, au katika kikao cha jimbo, kiburi kinaweza kusababisha taasisi au mtu binafsi kuwa mwasi, mwenye hasira, na mkaidi kwa sababu watu hawajawasikiliza. Kinachotakiwa ni unyenyekevu na kutambua kuwa mtu mmoja hana majibu yote. Fikiria kwamba bila shaka jumuia nzima, chini ya ushawishi wa Roho Mtakatifu, imeliongoza kanisa lote na kumngoja Bwana kwa ajili ya nuru zaidi. Hebu mtazamo wetu na uwe wa unyenyekevu na wa utiifu kwa Mungu katika Neno Lake kwanza, kisha kwa njia Zake alizoziweka za kutawala mahusiano yetu ya kibinadamu. Tukiwa pamoja katika lengo, tunaweza kutimiza utume wetu wa kufanya wanafunzi wa Yesu Kristo wanaoishi kama mashahidi Wake wenye upendo na kuwatangazia watu wote injili ya milele ya Ujumbe wa Malaika Watatu katika kujitayarisha kwa ajili ya kurudi Kwake upesi.

Ilikuwa mwishoni mwa Novemba 29, 1923, katika bweni la wavulana la Chuo cha Bethel huko Wisconsin, Marekani. Ernest Weaver, mlezi wa wanafunzi wa kiume, na mke wake Olive, muuguzi wa chuo, walisubiri kwa hamu kuzaliwa kwa mtoto wao mchanga, Arthur Willard. Dada mkubwa mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu, Wilma, alilala kwa utulivu katika chumba kilichopakana, kwa furaha bila kujua muujiza uliokuwa ukitokea nyumbani usiku huo.

 

Arthur alipokuwa na umri wa miezi sita, baba yake alikubali nafasi kama mkuu wa Chuo cha Fox River huko Sheridan, Illinois, Marekani. Waliendelea huko kwa miaka kadhaa. Arthur alipokuwa na umri wa miaka saba, baba yake alirudi masomoni, akajiandikisha katika Chuo cha Umishonari cha Emmanuel, ambacho sasa ni Chuo Kikuu cha Andrews.

 

Baada ya kumaliza masomo yake, Ernest alihamisha familia yake iliyokuwa ikiongezeka kwenda Ithaca, Michigan, Marekani, ambapo kulikuwa na shule ya kanisa karibu. Alitaka watoto wake wawe na elimu ya Kikristo, alidunduliza na kuhifadhi fedha ili hilo liwezekane. Baada ya mwaka mmoja huko Ithaca, Ernest alipokea simu ya kutumika kama mkuu wa Chuo cha Adelphian huko Holly, Michigan. Arthur alianza darasa la nne katika shule ya kanisa ya Holly.

 

 

MATAMANIO YA MWANZO

Tangu akiwa mdogo, Arthur alifahamu kwamba angekuwa daktari wa misheni. Anapeleka sifa hizi kwa wazazi wake waliomsomea visa vya utume. Mnamo Septemba 1941, alisajiliwa kama mwanafunzi wa awali wa udaktari katika Chuo cha Umishonari cha Emmanuel. Oktoba mwaka huo huo, alipokea barua kutoka kwa Rais wa Marekani, iliyomtaka kuhudumu katika mapambano ya Vita vya Pili vya dunia.

 

Januari 1942 alijiunga na mamia ya vijana wengine katika mafunzo ya msingi katika kambi ya Barkeley, Texas, Marekani. Alialikwa kuhudhuria shule ya mafunzo ya maofisa lakini alikataa, akijua kwamba angetarajiwa kubeba silaha. Kabla hajamaliza mafunzo ya msingi, Arthur alichaguliwa kwa ajili ya mafunzo ya dawa katika Hospitali Kuu ya Fitzsimmon huko Colorado. Akiwa huko alijifunza kutengeneza lihamu mbalimbali, dawa za kikohozi na zaidi.

 

Kapteni aliyesimamia programu ya dawa alimwambia Arthur kwamba ilikuwa programu ya siku 6 kwa juma. Arthur alipomwambia asingekuwepo siku za Jumamosi, Kapteni alijibu, “Huenda hutafanikiwa [katika programu hii], lakini unaweza kujaribu.” Kwa majaliwa ya Mungu, Kapteni alimpa Arthur ufunguo wa maabara siku za Jumapili ili kwamba aweze kufanya kazi za Jumamosi. Mwishoni mwa programu ya miezi mitatu, Arthur alipata alama ya juu katika kozi hiyo na kuchaguliwa kuwa Askari Bora katika kambi ya askari 5,000.

 

Kutoka katika hospitali ya Fitzimmons, Arthur alipelekwa San Francisco, California, Marekani, ambako, ijapokuwa alikuwa jeshini, alitumia miaka miwili na nusu kwenye meli iliyokuwa ikisafiri kote katika eneo la Pasifiki akipeleka na kuwaondoa askari katika maeneo ya mapambano. Wakati wa usambazaji wa askari wa Pasifiki, alipata likizo yake ya kwanza na aliweza kwenda nyumbani.

 

Usiku mmoja alipokuwa akiondoka, Arthur anasema, “Taa zilififia sebuleni kwa wazazi wangu na nilifikiri ni wakati mzuri wa kumwuliza mpenzi wangu Natalie Wheeker kama angekubali kuolewa nami. Nilivuta pumzi na kumwuliza, ‘Natalie, ungependa kunipikia maisha yako yote?’ Akajibu, ‘Mpenzi, ningependa kujaribu.’ ” Walifunga ndoa Juni 26, 1945, wakati wa likizo ya pili ya Arthur.

 

Arthur aliruhusiwa kuondoka kwa heshima kutoka katika Jeshi la Marekani mwezi Novemba 1945 na kujiandikisha katika kozi za udaktari katika Chuo cha Pacific Union Kaskazini mwa California. Baada ya miaka mitatu tu ya masomo, alisajiliwa katika Chuo cha Medical Evangelists, ambacho sasa ni Chuo Kikuu cha Loma Linda. Alipohitimu mwaka 1952, wenzi hao walirudi Michigan, Arthur akiwa kama daktari mkazi mwanafunzi na mpasuaji, ikifuatiwa na miaka mitano ya mazoezi ya upasuaji binafsi.

 

 

WATUMISHI WA KUJITOLEA

Katika majira ya joto ya mwaka 1960, Arthur alipokea mwaliko kutoka Konferensi Kuu kuhudumu kama daktari wa upasuaji wa misheni huko Karachi, Pakistan–jibu kwa ndoto yake ya utotoni. Mwezi Novemba, familia hiyo, ambayo sasa ilijumuisha watoto sita walio na umri wa chini ya miaka 12, ilipanda meli, ikitumia mwezi mmoja kusafiri na vitu vyao vya nyumbani na kufika Karachi Januari 1, 1962.

 

Arthur anasimulia, “Miaka hiyo mitano niliyokaa Pakistan nikiwa daktari mkuu wa upasuaji katika hospitali ya Waadventista wa Sabato huko Karachi, ambayo wakati huo ilitambuliwa kama hospitali kuu nchini humo, ilikuwa baadhi ya mambo hodari na yenye kuvutia maishani mwangu–baraka isiyo na kifani kwa familia yangu!”

 

Mwaka 1966, familia ya Weaver walirudi Marekani ambako Arthur alijiunga na kitivo cha Chuo Kikuu cha Jimbo la Wayne huko Detroit, Michigan, na kwa miaka 32 alifundisha upasuaji katika Hospitali ya Utawala ya Askari Mstaafu na Kituo cha Matibabu cha Detroit, huku akiendesha kliniki nyingi za Kuacha uvutaji wa Sigara.

 

Mwaka 1998, akiwa na umri wa miaka 75, Arthur alistaafu.

Hii ilimwezesha kuwekeza muda zaidi katika huduma. Kwa miaka mingi, Arthur na rafiki yake Dick Lane walipanga Safari za Utume za Maranatha, wakijenga makanisa Amerika ya Kati na Kusini. Arthur na Natalie walishiriki kikamilifu katika kupanga mikutano ya afya ya kila mwaka katika kituo cha Konferensi ya Michigan Au Sable ili kuwasaidia watu kuacha kuvuta sigara na kuboresha afya na mtindo wao wa maisha kwa ujumla. Familia ya Weavers walijulikana sana katika jamii kwa ukarimu wao.

 

Makala katika mwezi Desemba mwaka 1978 toleo la Gazeti la Ministry linalowahusisha wanandoa hao inaeleza:

 

“Dkt. Weaver alifanya vikao kadhaa vilivyotangazwa kote vya Mpango wa Siku Tano wa Kuacha Kuvuta Sigara katika eneo la Detroit. Natalie alikuwa na sifa ya upishi wa mboga mboga, kulingana na masomo yake ya upishi, hivi kwamba magazeti ya Detroit na vituo vya redio na televisheni mara moja vingeelekeza kwake watu ambao walionyesha kupendezwa na maisha yenye afya. Kwa hiyo, Familia ya Weaver walianza kuwaalika wageni nyumbani kwao kwa ajili ya chakula. Waliwaalika watu–mmoja au zaidi jioni–nyumbani kwao kwa muda wa majuma kadhaa. Kisha wakawaita na kuwaalika wajiunge na kikundi cha kujifunza Biblia cha madhehebu mbalimbali–ili kushirikishwa kwenye mlo wa bufee. Washiriki kadhaa wa kikundi cha mafunzo ya Biblia walibatizwa. 

 

Familia ya Weaver waliepuka kwa uangalifu kumshinikiza mtu yeyote kuchukua msimamo wake. Matokeo yalikuwa kwamba wale ambao hawakuwa wamefanya uamuzi bado walijisikia huru katika kundi. Na kwa kuwa mada nyingi zilikuwa za kuchagua wao wenyewe, waliendelea kujifunza Biblia na Bwana aliendelea kufanya kazi katika mioyo yao.”*

 

Baada tu ya Krismasi mwaka wa 2016, Natalie, mwenzi wa Arthur aliyejitoa mwenye umri wa miaka 72, alipata matatizo ya tumbo, na baada ya kukaa mwezi mmoja katika hospitali, alipumzika. Mwaka 2018, Arthur alioa mjane Mary Lou Ford Steinweg.

 

Mwezi Novemba 2023, familia na marafiki walisherehekea kwa furaha miaka 100 ya kuzaliwa kwa Arthur. Kwa kutazama nyuma juu ya maisha yake ya ajabu, anasema kwa kicheko, “Jambo kuu ninaloweza kusema, ni kwamba, mimi kati ya watu wote, nimebarikiwa zaidi! Kuanzia mwanzo hadi mwisho, lazima nimpe Mungu sifa kwa maisha marefu, yenye mafanikio, na maisha bora (na bado hayajaisha!).” Arthur na Mary Lou bado wako hai–wakimtumikia Bwana kupitia huduma kwa wafungwa, kwa njia ya barua za posta.

 

Urithi wa huduma wa Arthur umeenea kwa watoto wake na wajukuu ambao ni madaktari wa upasuaji, madaktari wa utabibu, wasaidizi wa madaktari, wafanyakazi wa kijamii, wasafishaji wa meno, wataalamu wa mwili, wauguzi, na waelimishaji.

Mtu anaweza kupata mifano mingi katika maisha na maandishi ya Ellen White ambapo karama ya unabii ilitumika kukuza umoja huu ndani ya kanisa-siyo tu kati ya washiriki wa kanisa lakini pia kati ya taasisi za kanisa letu. Moja ambayo haijulikani sana inahusisha ushuhuda ambao Ellen White aliandika mnamo mwaka 1899 kwa “mameneja na wasimamizi” wa nyumba zetu kuu sita za uchapishaji. Aliianza barua yake ya kurasa tisa kwa maneno haya:

 

Nimeshtushwa na roho ya ushindani ambayo inakuja katika nyumba zetu za uchapishaji. Inaonekana zaidi katika ofisi zetu kongwe zaidi za uchapishaji, lakini roho hiyo hiyo inafanya kazi mahali pengine. Roho hii, popote inapodhihirika, haimpendezi Mungu. Ikiruhusiwa kuwepo, itakua na kuimarika, na inapokua na kuimarika itaivunja roho ya umishonari. Itamhuzunisha Roho wa Mungu, na kuongoza katika njia ya kutenda ambayo itawafukuzia mbali kutoka kwenye taasisi na watenda kazi wake malaika wanaohudumu waliotumwa kufanya kazi pamoja na wale wanaoitunza neema ya Mungu.1

 

Je, ushuhuda huo wa wazi ulipokelewaje na viongozi wa nyumba zetu za uchapishaji? Katika angalau tukio moja, tunalifahamu jibu. Kisa kimesimuliwa na Henry Franz Schuberth.2 

 

 

KWA WAKATI TU

Henry alizaliwa mwaka 1868 nchini Ujerumani lakini akahamia Marekani ambako, katika miaka yake 20 ya mwanzo, alianza uhusiano wake na kanisa kama mwalimu wa Biblia na mwinjilisti wa vitabu kwa ajili ya Misheni ya Oakland huko California. Katika mkutano wake wa kwanza wa kambi, mnamo Septemba 1889, alitambulishwa kwa Ellen White na Mzee Nathaniel McClure, msimamizi wa utume wa mji huo. Alikumbuka Mama White akimuuliza, “Kama uko tayari kunisaidia, unaweza kutunza farasi na gari ambalo dada mmoja aliniazima nitumie nilipokuwa Oakland.” Henry alifurahi kufanya hivyo na mara nyingi aliendesha gari lake kwa ajili ya utembeleaji na ufanyaji shughuli wa Mama White.

 

Kama ilivyokuwa mara nyingi, Mama White alionyesha kupendezwa na siku za usoni za kijana huyu. Alimwuliza kama angependa kuhudhuria masomo yajayo ya Kijerumani ambayo yangefanyika katika Chuo cha Battle Creek. Alijibu kwamba alikuwa akiomba juu ya uwezekano huo, lakini hakuwa na fedha zilizohitajika. Baba yake alikuwa amemwondoa katika msaada wowote wa kifedha kwa sababu tu alikuwa anajihusisha na Waadventista.

 

Ellen White alijibu, “Haina shida; tutakutunza na kukupeleka Battle Creek.” Mama White alielekea huko kwa ajili ya Mkutano Mkuu wa Konferensi Kuu, na kwa vile masomo yasingeanza kwa majuma mengine matatu, Henry alialikwa kukaa nyumbani kwake. Aliandika kwamba uzoefu wake katika majuma ya mkutano huo “ulinigusa sana akilini mwangu kiasi kwamba sitausahau kamwe.”

 

Lakini tukirudi katika ushuhuda wa Ellen White wa 1899 kwa viongozi wa nyumba ya uchapishaji. Baada ya kumaliza elimu yake, Henry alifundisha katika Chuo cha Union huko Nebraska, kisha, mwaka wa 1894, akaombwa arudi Ujerumani na kuongoza shule ya mafunzo ya wanafunzi 15 iliyofunguliwa punde huko Hamburg, Ujerumani. Pia alipewa jukumu la Nyumba ya Uchapishaji ya Hamburg, pamoja na Mzee L. R. Conradi. Hapa tutaendelea na kisa kwa maneno ya Henry mwenyewe:

 

Kulikuwa na ugumu kidogo miongoni mwa watendakazi katika taasisi hiyo [nyumba ya uchapishaji]. Ilihusisha mpango wa kazi ya umishonari katika jiji baada ya saa za kazi. Nilikuwa nikiongoza katika mpango fulani na kuuhimiza. Ndugu mmoja alitofautiana sana na mapendekezo hayo, na wengine wakaungana naye. Roho ya utengano iliingia kwenye mikutano yetu, na hali ikatokea ambayo ilinitaabisha sana.

 

Jumapili fulani niliomba watumishi mbalimbali wa familia ya ofisi waje kwenye kikao katika kanisa siku ya Jumatatu jioni kwa ajili ya mkutano maalumu. Nilihisi kwamba lazima kwa njia fulani tutatue matatizo hayo. Jumatatu asubuhi, nilienda kwenye meza yangu. Kulikuwa na barua iliyokuwa na stempu za posta za Australia, yenye jina “E. G. White” iliyochapishwa kwenye kona. Nilifungua bahasha. Ndani yake kulikuwa na ujumbe kutoka kwa Mama White, unaohusu mambo yale yale yaliyoleta matatizo katika taasisi zetu.

Usiku huo kwenye kikao niliwauliza wafanyakazi, “Niliitisha kikao hiki lini?”

 

“Jana,” walisema.

 

“ ‘Vema,’ nikasema, ‘asubuhi ya leo nilipokea katika barua ujumbe wa Mama White kutoka Australia. Unahusu jambo lile lile ambalo nilitaka kuzungumza kwenu.’

 

“Nilisoma ushuhuda huo kwao, na kisha nikazungumza kwa maelezo yangu mwenyewe kwa ushauri uliotolewa ndani yake. Mara moja yule ndugu aliyesababisha tatizo hilo alisimama na kutoa mawazo yake mazuri ya Kikristo. Mmoja baada ya mwingine alifuata, na Bwana alitusaidia kutoka katika changamoto zetu.

 

“Sasa, mtu yeyote anaweza kufikiri kwamba kwa kuwa nilimfahamu Mama White, nilikuwa nimemwandikia barua huko Australia. Lakini katika siku hizo, ilichukua majuma sita kwa barua kutoka Hamburg kufika Australia, na changamoto yote hiyo ilikuwa imetokea ndani ya majuma matatu yaliyotangulia. Kwa hiyo ujumbe kutoka kwa Mama White ulitoka Australia yapata majuma matatu kabla ya changamoto kutokea Hamburg, na ulifika asubuhi tu ya siku hiyo nilipohitaji msaada.

 

Henry alimwandikia mara moja mtoto wa Ellen White, W. C. White, akionyesha shukrani zake kwa ajili ya maagizo ya wakati sahihi:

 

“Ndugu Mpendwa: Wako wa Septemba 25 na ushuhuda niliopokea asubuhi tu [kutoka kwa Mama White] nilipokusudia kutafuta ushuhuda wa kusoma katika kikao na watendakazi wetu. Nilikuwa nimepanga jioni ile ile kumtafuta Bwana; kwa hivyo ushuhuda huo ulikuja kwa wakati na umetusaidia wote na wote tulitambua kuwa ni kitu tu tulichohitaji na tunashukuru kwamba tuliweza kujiona katika nuru sahihi, kuungama kosa na kupokea msamaha.”3 

 

“Hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana mwana wa Mungu.” “Amina; na uje, Bwana Yesu!” (Efe. 4:13; Ufu. 22:20).

Kwa ufupi nitatoa muhtasari wa mamlaka ya Yesu wakati wa huduma Yake duniani, tatizo la ulimwengu mzima na uungu kuidhinisha mamlaka yote kwa Yesu.

 

 

MAMLAKA YA YESU 

Katika Mathayo, huduma ya Yesu ulimwenguni huonyesha udhihirisho wa daima wa mamlaka Yake. Ana mamlaka ya kufundisha (7:29) na hata mamlaka ya kusamehe dhambi (9:6, 8), akitazamia ukamilifu wa kazi Yake ya kuokoa kwa ajili yetu. Baadhi ya viongozi wa Kiyahudi walihoji mamlaka Yake (21:23), lakini kinyume chake, askari wa Kirumi alikiri hadharani kuwa Yesu alikuwa na mamlaka ya kuponya wagonjwa (8:5-13). Yesu Mwenyewe anatoa ushuhuda wa mamlaka Yake kufanya kazi kwa niaba ya wengine (21:27) na kwa bayana anatamka kwamba Baba amemkabidhi kila kitu Yeye–akiviweka chini ya mamlaka Yake (11:27). Ni dhahiri kwamba Yesu alikuwa na mamlaka aliyopewa na Mungu kabla ya kufufuka Kwake.

 

 

PAMBANO NA UTAWALA WA UUNGU

Wakati wa huduma Yake duniani, Kristo asingeweza kudhihirisha kikamilifu mamlaka Yake kwa ulimwengu wote. Sehemu ya uumbaji ilikuwa imekataa mamlaka ya Mungu ikidai uhuru kutoka Kwake. Yesu hakuwa na mamlaka kamili bado na sehemu hiyo ya uumbaji—uwezo wa kutumia nguvu Yake kuleta mabadiliko ya msingi. Aliwafundisha wanafunzi kuomba, “Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, duniani kama huko mbinguni” (6:10), lakini hilo lilikuwa bado halijatimia. Shetani alimjaribu Yesu ili amwabudu na awe mtawala wake juu ya falme za ulimwengu huu, lakini Yesu alimkemea tu (4:8-9). Mgogoro ulikuwa mkali kwa sababu Shetani alikuwa akipinga kazi ya Kristo kila wakati (13:19; 16:23). Pepo walitilia shaka mamlaka ya Yesu kuwazuia kufanya kazi yao wakidai kwamba hakuwa na, angalau kwa wakati huo, mamlaka ya kuwaangamiza (8:29; linganisha na Luka 4:34). Pepo walionekana kujua kwamba mabadiliko makubwa yalikuwa karibu kutokea.

 

 

KUANZISHA UPYA UTAWALA WA UUNGU 

Mambo yalibadilika kama matokeo ya kifo cha kafara ya Yesu. Sasa angeweza kutekeleza mpango wa Uungu wa kuhukumu ulimwengu mzima, kuwatenganisha wenye haki na waovu, kuwapa kila mmoja thawabu yao ya milele (25:31-46), na hatimaye kumwangamiza kabisa Shetani na pepo wake (Mathayo 8:29; 25:41). Sasa anaweza kutumia mamlaka Yake kuokoa na kuhukumu na kuangamiza waovu. Hakuna tena sehemu ya uumbaji nje ya mamlaka Yake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani” (28:18).

 

Kwa kutoa maisha yake kama fidia kwa wengi (20:28), alihalalisha mamlaka ya Uungu ya kuokoa wale wanaoweka imani yao Kwake (26:28; 25:34). Uadilifu wa tabia ya Mungu usingeweza tena kutiliwa shaka wakati wa kuokoa wenye dhambi (linganisha na Rum. 3:25-26) au kuhukumu wenye dhambi wasiotubu (Wafilipi 2:10-11; Ufunuo 5:13). Maneno ya Yesu baada ya kufufuka Kwake kwa wanafunzi yanajumuisha mawazo manne muhimu (Mathayo 28:18). Kwanza, Kristo alipokea mamlaka yote na hivyo hakuna mtu anayeweza kumpinga kama Bwana mtawala. Pili, Kristo sasa ni mtawala pamoja na Mungu, amevikwa taji kama mfalme mbinguni. Yeye ndiye mfalme wa Kimasihi; Mfalme wa wafalme. Tatu, anajitambulisha kwa wanafunzi kama Mpatanishi kati yao na Baba. Mamlaka aliyopokea Yesu kutoka kwa Baba anashiriki na wanafunzi wanapotangaza injili (Mathayo 28:19-20). Nne, neno “mbingu . . . dunia” linasisitiza muktadha wa ulimwengu mzima wa mamlaka ya Yesu. Hakuna kona ulimwenguni ambayo haitakuwa chini ya utawala wa upendo wa Mungu. Utawala huu utaonyeshwa kila mahali wakati wa kurudi kwa Kristo mara ya pili.

Kauli  kwamba “Hebu chakula kiwe tiba yako na tiba yako iwe chakula” mara kwa mara hufananishwa na dhana ya Hippocrates, mwanasayansi wa awali wa kiyunani, watatafiti wamechunguza kwa makini takwimu zilizopo na kauli hii haikuonekana katika maandishi yake.* Hippocrates anakazia umuhimu wa uhusiano uliopo baina ya Afya, chakula, mazoezi na dawa, lakini hachanganyi umuhimu na kazi ya  kila kimoja. Licha ya uhalisia, kauli hii ni kama panga likatao kuwili lenye vyote viwili ukweli na hatari kwa sababu inarahisisha sana sababu na madhara yake.

 

Lishe ni moja kati ya sababu kuu zinazoamua afya zetu na hali zetu njema. Lakini tunapotumia vyakula vyenye kalori nyingi, vyakula vilivyokobolewa sana, kutozingatia kiwango cha chakula na kunywa vinywaji  vyenye sukari nyingi  bila mipaka, tunatengeneza mazingira ya  kitambi au uzito uliopitiliza, shinikizo la juu la damu, kisukari namba 2, magonjwa ya moyo na hata kansa.

 

Sababu zingine zinajumuisha matatizo ya kijamii na uchumi, utunzaji wa afya na mazingira husika, sababu za kijenetiki, mazoezi, kupata usingizi, kutotumia pombe na tumbaku na tabia zingine hatarishi. Hizi zote huchangia umuhimu na ubora wa maisha. Uwepo wa vyakula bora, mahali penye hewa safi, na nafasi ya kufanya mazoezi salama kwenye eneo la wazi ni sababu zinazoelezea jinsi maisha marefu yanahusiana zaidi na postikodi moja kuliko sababu nyingine yeyote!

 

Tunaweza kuwaaibisha watu bila kukusudia tunaposema “upo hivyo ulivyo kwa sababu ya kile  unachokula” bila kutafakari mazingira ya mtu binafsi kama,  kutokuwepo kwa baadhi ya vyakula katika maeneo fulani, utunzaji mbaya wa chakula, kutopendeka kwa baadhi ya vyakula na kutokidhi gharama za utunzaji wa afya na  hali ya kutofautiana  kiuchumi iliyoenea ulimwenguni.

 

Tunahitaji kuufundisha ukweli na kushiriki ufumbuzi kwa upendo wa hali ya juu na huruma. Hii ni pamoja na kuelimishana jinsi ya kuchagua vyakula bora na sahihi kati ya vilivyopo, vyakula vyenye gharama nafuu na jinsi ya kuviandaa vyakula vyenye ladha nzuri na ya kupendeza. Makanisa ya Kiadventista yanaweza kuelezea mbaraka wa bustani za maua za jumuia na kupata hewa safi kwa yeyote anayeihitaji. Wenye busara hutumia chakula kukuza afya zao na kuzuia magonjwa yatokanayo na mtindo wa maisha.

 

Je lishe bora inaweza kutibu magonjwa? Kuondoa gluteni katika milo yetu kwa wale walio na mzio wa gluteni ni tiba rahisi kwa wale walio na tatizo hilo. Kwa kisiyeye, inayosababishwa na  upungufu wa asidi ya askobiki( vitamin C), ulaji wa mazao ya mti jamii ya michungwa na vyakula vingine vyenye wingi wa vitamin C ni matibabu. Lishe bora ya uangalifu na kuepuka vyakula vilivyosindikwa na wanga mwingi, ukijumuisha na mazoezi, kupungua uzito, udhibiti wa msongo na kuzuia na kuepuka mtazamo wa fedheha na kujilaumu “uliyasababisha haya wewe mwenyewe,” inaweza kuboresha hali na hata kuondoa kabisa aina ya 2 ya kisukari. Ulaji wa kiafya ni sehemu ya matibabu, pamoja na uhitaji wa dawa. Tunatakiwa kuelewa kwamba majaribio kupita kiasi ya kula kikamilifu kunaweza kusababisha athari zinazohusiana na kula. 

 

Jibu rahisi kwa swali lako: Lishe ni ya muhimu, Dawa ni za muhimu. Tunahitaji uwiano wa kinga, matibabu na kuishi vyema kiafya tukiwa na afya au tukiwa wagonjwa. Tuna fursa ya kudhihirisha upendo wa Mungu na kujali kwake, kushiriki na kukidhi mahitaji ya watu katika njia za kivitendo kama Yesu alivyofanya.  Kisha akawaambia wamfuate.  Nasi tufanye vivyo hivyo.

Nilitazama kimya uso wa Herb ukikosa tumaini. Kisha, mlio mkali wa sauti ya chini ukaondoa ukimya. “Hapana! Siyo miwani yangu!”

 

Tulikuwa tunasafiri kwenye Ghuba ya San Francisco, tukipita karibu na Kisiwa cha Alcatraz, kisha tukifuata upepo wa majira ya joto kuelekea Daraja la Golden Gate. Siku hiyo yenye mawingu huko California ilijumuisha upepo mkali, mawimbi makubwa, na urafiki wa kicheko.

 

Tulipita chini ya daraja pamoja na mashua zingine kadhaa, tukafurahia wakati mfupi katika bahari iliyo wazi, na kisha tukageuka kurejea kisiwa cha Angel.

 

 

KUTOKA FURAHA HADI JANGA

Rafiki wa chuo kikuu alikuwa amewaalika Baraza la Utawala la Chuo cha Pacific Union (ADCO) kujiunga naye katika siku moja ya safari kwenye mashua yake kubwa na nzuri. Dkt. Maxwell, rais wetu wa chuo, alikuwa ni baharia anayependa sana kazi yake na haraka akakubali. Kisha akatutaka wengi wetu kushiriki habari hiyo njema.

 

“Itakuwa Jumanne ijayo,” alisema, “na mtapenda hilo!”

 

Kwenye gati tulikuwa makini kusikiliza maagizo ya nahodha. Hayo yalijumuisha mahali pa kuvaa viokoa maisha majini, jinsi ya kutembea wakati mashua ipo katika mawimbi makubwa, jinsi ya kutumia choo, na wakati sandwichi ikiwa tayari.

 

Nimeelewa, nilifikiri, huku nikikaza jaketi langu wakati wa upepo wenye baridi.

 

Sikuwa nimewahi kwenda Kisiwa cha Angel, ingawa familia yetu ilikuwa imekwenda huko wakati wa safari ya baiskeli shuleni miezi kadhaa iliyopita. Kisiwa cha Angel ni kisiwa kikubwa zaidi katika Ghuba ya San Francisco na tangu miaka ya 1800 imehudumu kama kituo cha wahamiaji, na kama “kituo cha mwisho” kwa maelfu ya wanajeshi wa Vita vya II vya Dunia ambao walikuwa safarini kwenda kuvuka Pasifiki. Leo ni Hifadhi ya Jimbo la California pamoja na milima na fukwe zinazofaa kwa familia ambazo zinapenda baiskeli.

 

Tulikuwa tumeziacha baiskeli zetu nyumbani, lakini tulikuwa tunatarajia kutembelea majengo kadhaa ya zamani ya serikali baada ya kutia nanga Ayala Cove.

 

Wakati nahodha wetu alituleta taratibu kwenye gati, mmoja wa wasimamizi wetu, Herb Ford, aliruka chini kwenye gati inayokuwa ikiyumbayumba akisema angetusaidia kufunga kamba. Miguu ya Herb ilipogusa gati ya mbao, kila kitu kilisogea, na sisi wengine tukimwangalia bila msaada akitupwa kutoka kwenye gati na kuanguka ndani ya maji. Alipoibuka kutoka kwenye maji, sote tuliona kwamba miwani aliyokuwa amevaa usoni mwake kabla ya kuingia majini haikuwepo tena! Ilikuwa imetoka na sasa ilikuwa mahali fulani katika maji machafu ya Ghuba ya San Francisco!

 

Kwa muda fulani, siamini kama kuna mtu yeyote aliyepumua.

 

Kisha nikamwona Herb akitawaliwa na kukata tamaa badala ya tabasamu lake la kawaida. “HAPANA!” alinong’ona. “Siyo miwani yangu!”

 

Herb ni mwanafunzi, mwandishi na mtunzi wa maneno, mtu ambaye macho yake daima yanajishughulisha kukusanya rangi, maumbo na mawazo. Watu wengi “wanatazama.” Herb “huona.” Miwani yake ikiwa juu ya pua yake, huona vizuri. Bila miwani hiyo, Herb ni mtu aliyepotea.

 

Kila mjumbe wa ADCO mara moja alihisi maumivu ya Herb. Safari yetu ya mashua ilikuwa imegeuka kuwa janga.

 

 

JE, MUNGU ANAJALI?

Tulitazama chini ya upande wa mashua, tukitarajia kuona miwani ikiwa imekwama kwenye kamba au ikining’inia kwenye kipande cha mwani. Tulishuka chini kwenye gati, tukapiga magoti kwenye ukingo, na kufanya vivuli juu ya uso wa maji ili tuone vizuri zaidi. Tulizungumza na mtu aliyekuwa akikagua kibali chetu cha Hifadhi ya Jimbo.

 

“Kina cha maji chini ya mashua yetu ni kirefu kiasi gani?” tuliuliza. “Je, ni salama kiasi gani chini huko?” “Je, kuna papa yeyote?” “Je, una vifaa vyovyote vya kupigia mbizi ambavyo tunaweza kuazima?”

 

Majibu yake yalifanya hali kuonekana isiyowezekana. Hakukuwa na vifaa vya kupigia mbizi. Maji yalikuwa na kina cha takribani futi 12, yenye matope na baridi. “Hutaona chochote huko chini, na utahitaji mavazi ya kuzuia baridi ikiwa utapiga mbizi,” alikunja uso. “Samahani kuhusu hilo.” Kisha akarudi kazini.

 

Nikakaa kwenye gati, nikifikiri kuhusu miwani, Mungu na kuomba. “Je, Mungu hujali kuhusu miwani ya Herb?”

 

Wavuvi wawili walikuwa wakisafisha vifaa vya kuvulia ufukweni. Nilitembea kuwafuata, nikiwaza jinsi gani wangeweza kusaidia na ni nini nilipaswa kuwaomba. Njiani, Mungu alipendekeza niombe tena. Labda Anajali kuhusu miwani ya Herb, nilifikiri.

 

Bwana. Herb ni kipofu bila miwani yake. Ndiyo, anaweza kuona maumbo na vivuli, lakini si zaidi. Atahitaji miwani hiyo. Kwa kweli, anahitaji sasa hivi! Ikiwa kuna njia, tafadhali nionyeshe.

 

“Habari,” nilijaribu kusikika mwenye busara nilipowasalimu wavuvi. “Mmoja wa marafiki zangu amepoteza miwani yake karibu na gati. Kuna njia yoyote mnayoweza kumsaidia?”

 

Swali la kipuuzi, nilipaza sauti kujiambia.

 

“Oh hapana!” mmoja wao alisema kwa mshangao. “Sijui tunaweza kufanya nini, lakini tuna neli na miwani ya kupigia mbizi. Unaweza kuzitumia ikiwa utaamua kupiga mbizi na kutafuta.”

 

Mtu mwingine alijichekea. “Nina suti pia ya kuzuia baridi.” Taratibu alinipima kwa uangalifu kwa kutumia macho yake. “Nadhani unaweza kuvaa. Labda.”

 

 

KUPATA FUNZO

Sikutaka kupiga mbizi katika maji machafu karibu na gati ya Ayala Cove. Sikutaka kujibana kwenye suti ya kuzuia baridi iliyo ndogo sana kwa saizi mbili. Sikutaka kuchafua mikono yangu iliyokuwa safi kwenye matope na vitu visivyosemeka vinavyoweza kujificha chini ya gati. Sikutaka . . . 

 

Ninawaza kuhusu miwani ya Herb, Mungu alininong’oneza sikioni mwangu. Neli, barakoa na suti ya kuzuia baridi majini. Unahitaji nini zaidi?

 

Lakini, Mungu . . . Mazungumzo yangu yalionekana kuwa malalamiko zaidi kuliko maombi. Nilikuwa natarajia ungeifanya ielee, au kumtuma mtaalamu wa kupiga mbizi mwenye taa kubwa ya chini ya maji. Imekuwa miaka kadhaa tangu nipige mbizi baharini na sikupanga kupiga mbizi leo.

 

Wewe, Mungu alisema. Sasa.

 

Suti ya kuzuia baridi wakati wa kupiga mbizi ilihitaji kujibana na kutoa pumzi, lakini neli na barakoa vilikuwa sawa. Maji yalikuwa ya baridi, bila barafu. Uchafu ulikuwa mwingi zaidi kuliko nilivyofikiria. Nilipokuwa nikipembeza vidole vyangu toka upande hadi upande kupitia safu kubwa ya “baridi” chini, nilijaribu kutofikiria kupoteza mkono wangu kwenye chupa zilizovunjika au dragoni wa baharini.

 

“Hakuna kitu huko chini, Herb. Pole sana.”

 

“Tafadhali jaribu tena, Dick. Nitakuombea.”

 

Hakukuwa na chochote kwa mara nyingine, na sasa kikundi kidogo kilikuwa kikikusanyika kunitazama nikishindwa.

 

Bwana. Herb anahitaji miwani yake, nami nataka hii iwe mara yangu ya mwisho kupiga mbizi. Tafadhali tuma miwani kwangu.

 

Vidole vyangu vilipita katika kitu laini chenye kunata, kisha mkono wangu wa kulia ukagonga kitu kigumu na chembamba—na mikono ya kushikia! Nilishika kwa nguvu na kuelekea sehemu ya juu ya maji, mkono wa kulia kwanza. Wakati nilipoinua barakoa, Herb alikuwa akishusha mkono, akipiga kelele kwa sauti kubwa na kufikia kuchukua miwani yake mkononi mwangu.

 

Je, Mungu alijali kuhusu miwani ya Herb? Herb alifikiri hivyo. Wavuvi walifikiri hivyo. Afisa wa Hifadhi ya Jimbo alifikiri hivyo. Nahodha na wajumbe wengine wa ADCO walifikiri hivyo.

 

Mimi? Ninadhani Mungu alijua nilihitaji somo la kuamini Naye akanipatia, njia ya maji.

Mjomba mzee aliketi kimya akiutazama moto. Ilikuwa saa za jioni katika kijiji chake kilichopo Afrika na alikuwa peke yake katikati ya kundi dogo la vibanda. Taratibu, wanakijiji wenzake wakaanza kuungana naye. Walikuwa wamechoka kutokana na kazi ngumu za siku, lakini hakuna aliyetamani kutohudhuria tukio la jioni hii. Ulikuwa wasaa wa hadithi.

 

Kimya kilitawala kundi zima wakati Mjomba mzee alipoinua macho yake na taratibu kulitazama duara lote. Watoto walitetemeka kwa msisimko huku wakiwasogelea kwa karibu mama zao ili kupata joto. Je, huyu mjomba mzee atawasimulia hadithi gani jioni hii? Je atarudia mojawapo ya hekaya za wahenga? Au labda ataghani moja ya mashairi anayokumbuka. Wakati fulani aliwapa taarifa ya habari za ulimwengu. Nyakati zingine alieleza kwa umakini juu ya mmea, ndege, mdudu, au mnyama—akieleza anapoishi na namna ya kumtunza na kumtumia. Je, jioni hii itakuwa juu ya kitu gani?

 

Hatimaye, kila mtu alipokuwa amefika, Mjomba Mzee akasimama taratibu, akasafisha koo, “Hapo zamani za kale, msafiri alianza safari ndefu.”Aliposema maneno hayo, masumbufu ya siku yakaanza kutokomea taratibu kuelekea gizani, na kila mmoja akajiambia moyoni leo, “O, leo itakuwa ngano.”

 

Mjomba Mzee alikuwa msimulia hadithi mahiri, punde si punde mawazo ya kila mmoja yalikuwa yameanza kuhama kutoka kwake yeye, nyota, moto, na hata hewa baridi ya usiku. Badala yake walijikuta wakijikongoja kupitia mchanga wa moto wa jangwani katika safari hii ambayo Mjomba Mzee alikuwa akiwasimulia kwa maelezo bayana. 

 

Msafiri alikuwa ameondoka mapema, lakini joto lilikuwa limepanda sana. Yapata adhuhuri alijua kuwa tayari alikuwa matatani. Yawezekana kabisa kuna mahali alisahau njia na sasa alikuwa amepotea. Amepotea katika jangwa linalowaka moto.

Alipojaribu kuchukua tena kitu cha kunywa, aligundua kwamba maji yake yalikuwa yameisha, pia! Lo! Afanye nini sasa? Akakagua chupa zote kwa umakini, lakini zote zilikuwa tupu. Akatikisa chupa ili kupata tone la mwisho na kisha akaendelea kutembea. 

 

Aliendelea kujikongoja maili hata maili, akiwa hajui hasa anakokwenda, ila akijua kuwa ilimpasa kuendelea na mwendo au kufa kwa hakika. Mara akasimama. Hicho kilikuwa nini? Akafuta macho yake ili kuwa na uhakika kuwa haoni maruerue. Kwa mbali kulikuwa na mti, mti halisi. Huku akipumua kwa taabu, msafiri akaenda kasi kwa kadiri mwili wake uliokaukiwa maji ulivyomudu kwenda. Hatimaye, alipodhani asingeweza kupiga hatua nyingine aliufikia mti na kuanguka chini kwa kuishiwa nguvu chini ya uvuli wake.

 

Sasa, kama ni wa kufa, angalau angefia kivulini! Kisha, alipokuwa amelala pale, akasikia kitu fulani. Drip. Drip. Drip. Kilisikika kama maji! Aliinuka na kuketi sawasawa kisha akaangalia pande zote kwa shauku. Na, kwa hakika, kulikuwa na matone ya maji yakidondoka kutoka mtini kwenda mchangani.

 

Kwa haraka, msafiri akatoa kikombe chake kitupu cha maji na kukitegesha pale juu ya mchanga. Drip. Drip. Drip. Akalamba midomo yake. Hasha, bado alitaka kujizuia kuchukua kile kikombe cha maji. Alitaka kusubiri hadi kikaribie kujaa, ndipo ayanywe. Lakini ilikuwa vigumu sana kusubiri. Drip. Drip. Drip. Tena na tena, alinyosha mkono ili achukue kikombe, na kisha akaurudisha mkono wake.

 

Sasa. Bado matone machache tu ili aweze kunywa. Naam. Kikajaa. Lakini alipojaribu kuchukua kikombe, kitu fulani kikapita mara kutokea mtini, kikagonga kikombe, na kumwaga maji haya ya thamani juu ya mchanga mkavu wa jangwani.

 

Haiwezekani!” alimlalaikia ndege aliyeruka na kuangusha kikombe chake cha maji.

Machozi ya moto yanayotokana na hasira na kukata tamaa yakatiririka katika mashavu yake. Alidaka kikombe kwa nguvu na kukisimika tena mchangani. Drip. Drip. Drip. 

 

Mara hii akaamua kufanya ulinzi. Na hatimaye, kukasalia matone machache ili apate kunywa. Loo! Ndege akaruka kutokea upande mwingine, akadondosha kikombe na kurejea mtini.

 

Akipiga kelele kwa hasira, mtu yule akakisimika kikombe tena. Drip. Drip. Drip. 

 

Mara nne zaidi, kadiri kikombe kilipokaribia kujaa, ndege aliruka toka mtini kupitia miguuni pake, chini ya mikono yake, akamwaga yale maji kabla yule msafiri hajayanywa. Mara hii, huyu msafiri mwenye hasira akaona jiwe kubwa kwa karibu. Kwa mara ya saba akasimika kikombe. Mara hii akasimama mwenyewe akiwa ameinua jiwe juu zaidi ya kichwa chake. Alisikia tu kwa mbali matone ya maji yakidondoka drip, drip, drip. Aliona tu kwa mbali kuwa kikombe kilikuwa kikijaa taratibu. Badala yake aliinua jiwe akiwa tayari. Na kwa hakika, kikombe kilipokaribia kujaa, ndege aliruka na kumwaga maji tena.

 

Aaaggghhhh!” alipiga kelele yule msafiri wakati akirusha jiwe kumwelekea ndege yule aliyekuwa akitokomea. Jiwe likampiga yule ndege na kumdondosha chini. Yule msafiri akajiambia kuwa “yawezekana sasa nitapata kitu cha kunywa.” Lakini mara aliposimika kikombe akagundua kitu. “Haiwezekani,” alipaza sauti yake. “Hayawezi kukoma kwa sasa!” Lakini matone ya maji yalikuwa yamekoma kabisa kudondoka!

 

Huku akilia na kupiga kelele kwa hasira, yule mtu akadondoka chini na kusema kikwifukwifu. Kisha mara akanyamaza. Nini hicho? Juu yake tu? Kwenye mti ambapo maji yamekuwa yakidondoka kutokea? Joka mkubwa. Meno yake yenye sumu yalikuwa juu ya mahali pale ambapo sumu ya kufisha ya nyoka ilikuwa ikidondokea katika kikombe chake. Ndipo yule msafiri akajua kuwa yule njiwa mdogo alikuwa ameokoa maisha yake. Naye alikuwa amemuua!

 

Kimya kimya, yule Mjomba Mzee akatembea taratibu kutoka kwenye mwanga wa moto uliokuwa ukiwaka. Hakuna aliyesogea. Walikuwa wamezama katika kutafakari juu ya fundisho la hadithi hiyo.

 

*****

 

“Niliposikia hadithi hii kwa mara ya kwanza kama mvulana mdogo kijijini,”rafiki yangu Peter aliponiambia, “sikuweza kung’amua ilichomaanisha. Lakini sasa kwa kuwa mimi ni Mkristo, ninajua. Kuna nyoka wa zamani aitwaye ibilisi na Shetani anayezungukazunguka akijaribu awezavyo kutuangamiza. Yesu alituokoa toka kwa sumu ya yule “nyoka” nasi tulimgongomelea msalabani wakati akijaribu kutuokoa!”

 

Peter aliendelea huku akitabasamu, “Lakini namshukuru Mungu kuwa hadithi hii ina mengi kuliko kile Mjomba Mzee alichotuambia. Yesu hakutufia tu. Alifufuka toka kaburini! Yu hai! Na anarudi tena kutuokoa.”

Mchapishaji

Jarida la Adventist World, jarida la kimataifa la Kanisa la Waadventista wa Sabato. Konferensi Kuu, Divisheni ya Asia Pasifiki ya Waadventista wa Sabato ndio wachapishaji.

 

Mkurugenzi Mtendaji/ Mkurugenzi wa Huduma za Adventist Review

Justin Kim

 

Meneja wa Uchapishaji wa Kimataifa

Hong, Myung Kwan

 

Kamati ya Uratibu ya Jarida la Adventist World 

Yo Han Kim (chair), Tae Seung Kim, Hiroshi Yamaji, Myung Kwan Hong, Seong Jun Byun, Dong Jin Lyu

 

Wakurugenzi wenza/ Wakurugenzi, Huduma za Adventist Review

Sikhululekile Daco, John Peckham, Greg Scott

 

Wahariri waliopo Silver Springs, Maryland, Marekani

Enno Müller, Beth Thomas

 

Wahariri waliopo Seoul Korea
Hong, Myung Kwan; Park, Jae Man; Kim, Hyo-Jun

 

Mkurugenzi wa Mambo ya Kidijitali

Gabriel Begle

 

Mkurugenzi wa Muungano wa Mifumo na Uvumbuzi

Daniel Bruneau

 

Meneja wa Shughuli

Merle Poirier

 

Mratibu wa Tathmini ya Uhariri

Marvene Thorpe-Baptiste

 

Wahariri /Washauri wengine

E. Edward Zinke

 

Meneja wa Fedha

Kimberly Brown

 

Mratibu wa Usambazaji

Sharon Tennyson

 

Mratibu wa toleo la Kanda (Adventist World)

Penny Brink

 

Bodi ya Utawala

Yo Han Kim, chair; Justin Kim, secretary; Hong, Myung Kwan; Karnik Doukmetzian; SeongJun Byun; Hiroshi Yamaji; Joel Tompkins; Ray Wahlen; Ex-officio: Paul H. Douglas; Erton Köhler; Ted N. C. Wilson

 

Maelekezo ya Usanifu na Muundo

Types & Symbols

 

Kamati ya Adventist World ya Divisheni ya Afrika Mashariki – Kati:

Blasious Ruguri, Musa Gideon Mitekaro, Tom Ogal, Emanuel Pelote.

 

Tafsiri

Ufunuo Publishing House, South Tanzania Union Conference.

 

Msomaji wa prufu

Lilian Mweresa

 

Usanifu wa toleo la Kiswahili

Daniella Batista, Ashleigh Morton, Digital Publications

 

Uchapishaji wa Kidijitali

Charles Burman, Digital Publications (www.digitalpublications.co.za)

 

Muelekeo wa Sanaa na Ubunifu

Mark Cook, Brett Meliti, Ivan Ruiz-Knott

/Types & Symbols

 

Kwa Waandishi: Tunakaribisha miswada huria. Tuma barua zote kwa uhariri kwa 12501 Old Columbia Pike, Silver Spring, MD 20904-6600, U.S.A. Faksi ya ofisi ya Uhariri ni: (301) 680-6638

 

Waraka pepe: worldeditor@gc.adventist.org

Tovuti: www.adventistworld.org

 

Rejea zote za Biblia zimechukuliwa kutoka kwenye Swahili Union Version Bible Toleo la Chama cha Biblia la mwaka 1952.

 

Jarida la Adventist World linachapishwa kila mwezi na kuchapwa kwa wakati huo huo huko Korea, Brazili, Indonesia, Australia, Ujerumani, Austria, Ajentina, Meksiko, Afrika Kusini, na Marekani.

 

Vol. 20, Na. 3

Swipe left

swipe left To move to the next page

Swipe right

swipe right To move to the previous page
Allow Send-it to use cookies?

Send-it uses cookies to track how you use the application. Find out more about what data we collect and how we use the data in our privacy policy.